Siku
ya leo yaani tarehe 19.11. ni siku maalumu na ya kumbukumbu ulimwenguni
kote kwa wapenda amani na maendeleo ya jamii, wapigania amani na haki
za binadamu. Ni siku ambayo alizaliwa mwanazuoni Idrissa Abdallah
Majura, tarehe 19.11.1938 katika kijiji cha Gera, Mkoani Kagera nchini
Tanzania. Ndugu Majura alikuwa miongoni mwa wanafunzi wachache toka
Tanganyika wakati huo waliobahatika kupata scholarship ya kwenda
masomoni huko Zanzibar. Baada ya kufuzu masomo yake alitunukiwa shahada
ya Elimu na kuwa mwalimu katika shule na vyuo mbalimbali Kisiwani
Unguja. Mbali na uwanja wa Elimu Idrissa Majura alikuwa mwana michezo
hodari aliyeichezea timu ya Taifa ya Zanzibar akiwa golikeeper mashuhuri
wakati huo. Pia alikuwa mwanariadha hodari sana ambaye rekodi zake
hazijavunjwa hadi leo!! Idrissa Majura alikuwa mpenzi wa watu wengi huko
Kisiwani Unguja. Ingawa hakujihusisha na mambo ya kisiasa, kama
wananchi wengine wa Zanzibar aliyaunga mkono mapinduzi yaliyomungòa
Sulatani na kuleta uhuru kwa wananchi wote Visiwani. Watu wengi huko
Unguja na Pemba walimpenda sana na alifahamiana na watu wa chini na
wakuu pia. Ingawa aliishi muda mrefu huko Zanzibar, hakusahau nyumbani
kwao huko Bukoba. Kila mara alikuwa akija likizo kuwaona wazazi wake,
jamaa na ndugu zake. Alitoa misaada mingi kwa kuwasomesha wanafunzi
wengi wa Mkoa wa Kagera na Tanzania kwa ujumla. Mnamo mwaka 1969
aliamua kufuta kazi na kurejea nyumbani ili awe karibu na wazazi wake
waliokuwa wameanza kuzeeka. Ndipo balaa lilipomkuta muda mfupi baada ya
kurejea nyumbani, akakamatwa kwa visingizio kuwa alishiriki kwenye njama
za kutaka kuiangusha serikali ya Mapinduzi ya Abedi Amani Karume. Kwa
sababu ambazo hazieleweki, Serikali ya Mwungano ilikubali arejeshwe
Zanzibar, ingawa ilijua wazi kuwa kufanya hivyo ilikuwa ni kumweka
kitanzi, kama Wazanzibari wengine walivyouawa kwa ukatili wakati huo. Ni
wazi kabisa kuwa Idrissa Majura hakuwa mwanasiasa na wala hakujihusisha
na madai ya uongo yaliyotolewa kuwa alitaka kuipindua serikali ya
mapinduzi. Wakati huo wa kutisha huko Visiwani, kila aliyekuwa na Elimu
au kutoa kauli yoyote ya kumpinga Karume, hatima yake ilikuwa ni kukiona
cha mtema kuni – yaani kifo au kifungo cha maisha. Mpaka leo
haijulikani mwanazuoni huyo aliuawa vipi ? na kuzikwa wapi ?, kwani
hakufikishwa mahakamani ili ajitetee na kuhukumiwa. Vyombo vingi vya
kimataifa vimeanza kuulizia suala hili na tuna imani siku itafika ambapo
ukweli utajulikana. Mola aiweke roho yake mahali Pema Peponi - Amin
0 Comments
unashauriwa kutoa maoni muda na wakati wowote na kama unahabari yeyote unaruhusiwa kututumia