Ticker

6/recent/ticker-posts

ACT KUTISHIA UKAWA KWA KUWAARIBIA KURA



Huenda mpango wa vyama vinavyounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa), kufanya vizuri katika Uchaguzi Mkuu wa Oktoba, ukatibuliwa kufuatia tishio lililopo la chama kipya cha siasa cha ACT.
Duru za siasa zinakitazama Chama cha ACT chini ya Zitto Kabwe aliyefukuzwa Chadema hivi karibuni, kama tishio kubwa kwa upinzani nchini. Ni chama  kinachoweza kusababisha CCM iendelee kuwa kinara katika chaguzi za Tanzania.
Zitto, mwanasiasa machachari aliyejiunga na ACT, anatajwa kujijengea ngome katika baadhi ya maeneo yanayotegemewa na Ukawa, jambo linaloelezwa na baadhi ya wachambuzi wa masuala ya siasa kuwa  huenda likazorotesha nguvu ya upinzani, endapo chama hicho kichanga katika siasa kitaamua kusimamisha wagombea katika maeneo hayo.
Baadhi ya mikoa inayoonekana kuwa tegemeo kwa upinzani chini ya Ukawa na ambayo Zitto anaonekana kujenga himaya yake,  ni pamoja na mkoa wa Kigoma wenye zaidi ya majimbo sita ya uchaguzi ambayo yanategemewa  na upinzani.
Mikoa mingine ni Mtwara, Lindi, Shinyanga, Kagera, Katavi, na Sumbawanga.
Kwa Kigoma majimbo yanayotajwa kuwa hatarini kumezwa na ACT yanatajwa kuwa ni pamoja na Kigoma Mjini, Kigoma Kaskazini, Kigoma Kusini, Muhambwe, Kasulu Vijijini na Kasulu Mjini.
Majimbo mengine ambayo ACT inaonekana kuwa na ushawishi na inaweza au kuyatwaa au kusababisha Ukawa kukosa ushindi ni pamoja na Mpanda na Sumbawanga Mjini.
Zitto ajigamba
Katika kudhihirisha amejipanga vyema kushiriki Uchaguzi Mkuu ujao na kufanya vyema kupitia ACT ambacho kwa muda mrefu amekuwa akihusishwa kukiasisi, Zitto anasema:
“Mimi ni mchapakazi, siangalii nyuma tena, naangalia mbele. Mapambano yanaanza, matokeo mtayaona baada ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka huu.”
Alitoa majigambo hayo alipotangaza kujiunga rasmi na chama hicho mwishoni mwa wiki, huku akiwa na kundi la watu waliowahi kuwa wanachama na viongozi wa Chadema.
Swali kuu ni; je, ACT kikiwa katika hatua za uchanga, kinaweza kuleta ushindani katika uchaguzi?

Post a Comment

0 Comments