Ticker

6/recent/ticker-posts

WANANCHI MASASI WAILALAMIKIA TANESCO KWA KUKATA UMEME MARA KWA MARA




Na Dotto Mwaibale, Masasi

WANANCHI wa Wilaya ya Masasi Mkoani Mtwara wamelilamikia Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) kutokana na kuwakatia umeme mara kwa mara na kusabisha kuwaunguzia vifaa vyao vya majumbani na kuwa hadha kwao.


Wakizungumza na waandishi wa habari wilayani hapa leoa wananchi hao walisema kuwa tabia hiyo ya kukatiwa umeme mara kwa mara imekuwa sugu na hawajui kilio chao hicho wakipeleke wapi.

" Hii tabia ya kukatiwa umeme kila siku tena bila ya kupewa taarifa imekuwa sugu hapa wilayani kwetu hatuji ni nani tumuambie" alisema Muharami Hamisi mkazi wa mjini hapa.

Hamisi alisema wananchi wengi wamekuwa wakiunguliwa vifaa vyao vinavyotumia umeme zikiwemo taa lakini wanakaa kimya kwa kuwa hajui wapi waende kulalamika.

Mwajabu Liganga alisema wanaona kama Tanesco wanawafanyia makusudi kuhusu kukatika huko kwa umeme kwa mara kwa mara kwani wanapofika viongozi wa kitaifa katika mji huo huwa hawakati umeme unawashwa kuanzia asubuhi hadi jioni.

"Tunashangaa wanapofika viongozi wa kitaifa hapa wilayani umeme haukatwi lakini wakiondoka tu hali inarudi palepale" alisema Liganga.

Liganga aliongeza kuwa umeme huo kwa siku umekuwa ukikatwa na kuwashwa kwa zaidi ya mara kumi bila ya kuwepo kwa maelezo ya kina.

Akizunguzia madai hayo Ofisa Usambaji wa Umeme wa Wilaya hiyo aliyetajwa kwa jina la Iddi Kuhanga alikiri kuwepo kwa changamoto hiyo akieleza kuwa sababu kubwa ni uwezo wa uzalishaji wa umeme huo kuwa mdogo.

Alisema kuwa umeme unaotumika wilayani hapo unatoka mkoani Mtwara hivyo hadi ufike  Masasi unakumbana na changamoto nyingi ikiwemo ya kuharibiwa kwa miundombinu kwa kuangukiwa na miti kutokana na shughuli za kilimo au ndege kukaa kwenye nyaya.

Kuhanga alikanusha madai ya kuwa wanapofika viongozi wa kitaifa hali hiyo ya kukatika umeme huo inakuwa haipo.


Post a Comment

0 Comments