POLISI WA UJERUMANI WAMKOSA KABUGA 2007,MWENDESHA MASHITAKA NORWAY ATAKA MTUHUMIWA AFUNGWE MIAKA 21 JELA

Jarida moja la kila wiki la Ufaransa limechapisha habari kwamba polisi nchini Ujerumani walimkosa kumtia mbaroni mwaka 2007, mtuhumiwa wa mauaji ya kimbari ya Rwanda anayesakwa vikali, Felician Kabuga huku Mwendesha mashitaka nchini Norway ameiomba mahakama impatie kifungo cha miaka 21 jela mfanyabiashra mmoja wa Rwanda kwa kushiriki kwake katika mauaji ya kimbari mwaka 1994.
NORWAY
Ataka mtuhumiwa wa mauaji ya kimbari afungwe miaka 21: Jumatatu wiki hii, mwendesha mashitaka nchini Norway ameiomba mahakama impatie kifungo cha miaka 21 jela mfanyabiashara mmoja wa Rwanda,Sadi Bugingo, iwapo atatiwa hatiani kwa mashitaka ya kula njama za kuua watu 2,000 nchini mwake mwaa 1994.Pamoja na mambo mengine anashitakiwa kwa kudaiwa kushiriki katika mikutano ambayo mauaji hayo yalipangwa na hatimaye kutekelezwa.Mwendesha mashitaka iliiambia mahakama kwamba hakuna sababu zilizotolewa kuomba punguzo la adhabu iliyopendekezwa.
UFARANSA
Polisi wakosa kumtia mbaroni Kabuga: Jarida moja la Ufaransa Jumanne wiki hii limeripoti kuwa polisi nchini Ujerumani mwaka 2007 walimkosa kumtia mbaroni mtuhumiwa wa mauaji ya kimbari anayetafutwa vikali, Felicien Kabuga.Kwa mujibu wa jarida hilo la kila wiki la Ufaransa, Jeune Afrique, Kabuga, anayedawa kuwa mfadhili wa mauaji ya kimbari ya Rwanda ya mwaka 1994, aliingia nchini Ujerumani kwa kutumia hati bandia ya kusafiria ya Tanzania.Imeripotiwa kwamba mshitakiwa huyo alikwenda nchini Ujerumani wakati huo kwa ajili ya kupata matibabu ya maradhi ya kupumua yaliyokuwa yanamsumbua.
Mahakama Ufaransa yanadai jalada la kesi ya Waziri wa Rwanda lina utata: Mwendesha mashitaka katika Mahakama ya Rufaa mjini Paris, Ufaransa amedai Jumatano kwamba kumbukumbu za waziri wa zamani wa Rwanda, anayetakiwa nchini mwake, Hyacinthe Rafiki Nsengiyumva limekosa ufafanuzi na kukiuka taratibu zinazotakiwa na mahakama. Pamoja na mambo mengine taratibu zilizokiukwa ni pamoja na Mwendesha mashitaka mmoja kutia saini hati ya mashitaka na hati ya kukamatwa kwa mshitakiwa huyo. Lakini akijibu hoja hiyo, Mwendesha Mashitaka Mkuu wa Rwanda, Martin Ngoga, amelezea kuwa maoni kama hayo ni kiburi cha hali ya juu. Nsengiyumva alitiwa mbaroni mjini Paris,mwaka 2011, kufuatia hati ya Rwanda iliyomtaka mshitakiwa huyo iliyotolewa 2008.
RWANDA  
Jallow akabidhi Rwanda jalada la Munyarugarama: Mwendesha Mashitaka wa Taasisi itakayorithi kazi za Mahakama mbili za Kimataifa, Hassan Bubacar Jallow, Jumatano alikabidhi jalada la mshitakiwa ambaye bado hajatiwa mbaroni, Kanali Pheneas Munyarugarama kwa Mwendesha Mashitaka Mkuu wa Rwanda, Martin Ngoga.  Sherehe hizo za makabidhiano zilifanyika mjini Kigali.Munyarugarama ambaye alikuwa Kamanda wa kambi ya jeshi ya Gako, katika mkoa wa Kigali Vijijini, anashitakiwa kwa mashitaka ya mauaji ya kimbari, kula njama za kufanya mauaji hayo, uchochezi na uhalifu dhidi ya binadamu.
WIKI IJAYO
Kesi ya Bemba kuendelea kuunguruma wiki ijayo: Kesi ya utetezi inayomkabili kiongozi wa zamani wa Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo (DRC), Jean Pierre Bemba anayeshitakiwa kwa uhalifu dhidi ya binadamu na uhalifu wa kivita itaendelea kusikilizwa Jumatatu ijayo, Desemba 3,mbele ya Mahakama ya Kimataifa ya Makosa ya Jinai (ICC). Uhalifu huo unadaiwa kufanywa kati ya mwaka 2002 na 2003 katika Jamhuri ya Afrika ya Kati.

About Woinde Shizza

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 Comments:

إرسال تعليق

unashauriwa kutoa maoni muda na wakati wowote na kama unahabari yeyote unaruhusiwa kututumia