Ticker

6/recent/ticker-posts

POLISI YATOA SOMO KWA VIONGOZI WA SERIKALI ZA MITAA

  Mkuu wa Polisi Jamii mkoa wa Arusha Mkaguzi wa Polisi Shabani Shabani akitoa ufafanuzi juu ya sheria ndogo ndogo zinazoweza kumbana mtu atakayekaidi kulipa michango ya ulinzi shirikishi katika eneo lake

Diwani wa kata ya Moivaro Bw. Rick Moiro akichangia jambo katika mkutano uliokuwa unazungumzia juu ya ulinzi shirikishi katika kata yake
Viongozi wa kata na mitaa wametakiwa kutoumiza vichwa vyao na kuvutana mashati na wananchi watakaokaidi kutoa michango katika masuala ya ulinzi na badala yake wanatakiwa wawabane kwa kutumia sheria.

Akizungumza jana katika mkutano uliofanyika mtaa wa Moshono Kaskazini kata ya Moivaro tarafa ya Suye halmashauri ya jiji la Arusha, Mkuu wa Polisi Jamii mkoa wa Arusha, Mkaguzi wa Polisi Shabani Shabani aliwaambia viongozi pamoja na wananchi kuwa wanaweza kutunga sheria ndogo ndogo kupitia sheria ya serikali za mitaa ya mwaka 2000.

“Hakuna haja ya kuumiza kichwa bali viongozi mnapaswa kutumia kifungu namba 163 na 164 katika kitabu hicho wamezungumzia namna ya kutunga sheria ndogo ndogo kulingana na mahitaji ya eneo lenu”

“Lakini pia kifungu namba 167 kinazungumzia adhabu zinazoweza kutolewa kwa mtu yeyote ambaye hatashiriki au atakayeshawishi kukwamisha masuala ya ulinzi atatozwa faini ya Shilingi 50,000”. Alifafanua Mkaguzi huyo wa Polisi Shabani Shabani.

Alisema pia mbali na kitabu hicho cha sheria pia katika ibara ya 27 na 28 za katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania zinazungumzia wajibu wa kila mtanzania juu ya ulinzi wa mali za umma pamoja na kulilinda Taifa hivyo aliwataka viongozi hao wafanye kazi zao kwa kujiamini na wafahamu kwamba sheria juu ya hilo zipo wazi.

Alizidi kuhamasisha viongozi hao kufufua kikundi cha ulinzi shirikishi ambacho kinaonekana kusimama katika uteketezaji wa majukumu yake, na kutoa mifano ya baadhi ya kata zilizopo halmashauri ya jiji la Arusha ambazo zimepiga hatua kubwa katika kuimarisha vikundi hivyo vya ulinzi shirikishi ambapo wana sare pamoja na silaha za moto na kuongeza kwamba hali hiyo inatokana na hamasa ya wananchi wenyewe.

Alisema vikundi hivyo vina faida kubwa katika suala zima la kuimarisha ulinzi hasa ikizingatiwa kwamba askari wa Jeshi la Polisi wao pekee hawatoshelezi kusambaa kila mitaa kwa mara moja kutokana na idadi yao kuwa ndogo kauli ambayo iliungwa mkono na Mwenyekiti wa mtaa huo Bi. Janeth Jonas.

Akichangia wazo katika mkutano huo Diwani wa kata ya Moivo Bw. Rick Moiro alisema pamoja na utaratibu wa kuwatambua na kuwabainisha wahalifu kwa njia za siri kuendelea katika kata hiyo, lakini akasema ni vyema Jeshi hilo likaanza kuwakamata wahalifu wanaojulikana badala ya kusubiri mpaka orodha ya wahalifu wengi ipatikane.

Akijibu malalamiko ya wananchi hao waliohudhuria kikao hicho juu ya baadhi ya askari wa vikundi shirikishi hao kutoonekana mitaani wakati wa usiku kwa madai kwamba huwa wanakwenda kulala, Mtendaji wa Kata hiyo Bw. Goodluck Anderson alisema kwamba kwa sasa wananchi waondoe hofu na kuahidi kulisimamia jambo hilo kwa ukaribu zaidi ili kuweza kubaini ukweli wa malalamiko hayo.

Post a Comment

0 Comments