Ticker

6/recent/ticker-posts

VYAKULA VITANO MUHIMU KWA UKUAJI WA AKILI YA MTOTO


Na Jumia Food Tanzania

Miongoni mwa changamoto zinazowakumba wazazi wengi wa kitanzania ni kushindwa kufahamu na kupangilia vyakula sahihi kwa ukuaji wa afya za watoto wao. Afya ya akili ya mtoto ni kitu muhimu na cha kuzingatia kwani humfanya mtoto aweze kufanya shughuli tofauti kwa ukamilifu ikiwemo uwezo wake wa kujifunza shuleni pamoja na kushiriki michezo mbalimbali na wenzake.
Baadhi ya wazazi kwa kutokufahamu huwapatia watoto wao vyakula ambavyo huwa haviwasaidii watoto kwenye hatua ya ukuaji. Inawezekana watoto huwa hawapendelei vyakula hivyo muhimu kwa afya zao, lakini inashauriwa kuanza taratibu na hatimaye wanazoea. Jumia Food imekukusanyia aina tano za vyakula ambavyo ukianza kumpatia mtoto wako utashangazwa na ukuaji wa afya ya akili yake.

Mayai. Virutubisho vinavyopatikana kwenye mayai ni muhimu kwenye utengezaji wa seli zinazotunza kumbukumbu kwenye ubongo. Kadiri tunavyokuwa na seli nyingi ndivyo tunakuwa na uwezo mkubwa wa kuhifadhi kumbukumbu. Hivyo ni vizuri kuzingatia kujumuisha aina hii ya chakula unapomtayarishia mtoto wako chakula, kwa mfano asubuhi kabla mtoto hajakwenda shuleni.  

Maziwa. Maziwa yasiyo na mafuta yanajulikana kuwa chanzo kikubwa cha protini, Vitamini D na fosforasi. Lakini pia kalsiamu inayopatikana ndani yake inasaidia namna miili yetu inavyodhiti nishati. Kalsiamu pia ina mchango mkubwa kwa uzalishaji wa insulini kwenye miili yetu. Mbali na kunywa maziwa kama yalivyo unaweza kunogesha kwa kuongeza chokoleti. Wataalamu wanasema kwamba kuna kiasi kidogo cha ‘kafeini’ kwenye maziwa ya chokoleti, na yanakuwa karibu na kiasi sawa cha sukari iliyopo kwenye juisi za matunda.  

Matunda. Ukuaji wa afya ya akili ya mtoto huhitaji matunda kwani humsaidia kwenye mchakato mzima wa kujifunza. Lakini pia matunda husaidia katika mchakato mzima wa kulainisha choo hivyo kusaidia kwa kiasi kikubwa watoto wengi wanaokumbwa na changamoto hiyo. Ukiachana na maji na mazoezi, matunda ni mbinu bora ya kuwafanya watoto kuwa na afya bora na hivyo akili kuwa tayari kwa kujifunza. Ili kutomtia mtoto uvivu katika kula matunda, unaweza kumuandalia kwa kuyakata kwa mtindo wa vipande vidogovidogo.   
Maji. Jambo ambalo wazazi wengi hawalifahamu ni ambavyo watoto wao hunywa kiasi kidogo sana cha maji kutwa nzima. Wataalamu wengi wamekuwa wakionya namna maji ambavyo huwa yanapuuzwa kama chakula muhimu kwenye mwili wa binadamu, si kwa watoto tu bali hata watu wazima. Watoto muda mwingi huwa wanakuwa kwenye pilikapilika zao bila ya kuwa na maji ya kutosha mwilini. Kutokunywa maji au kutumia kwa kiasi kidogo huwafanya watoto kuhisi njaa isiyo ya lazima. Hakikisha kuwa unajumuisha maji kwenye kila mlo unaomuandalia mtoto wako.
Nyama. Ukosefu wa madini ya chuma ni miongoni mwa tatizo sugu linalotokana na upungufu wa lishe, na huongoza kwa magonjwa yanayotokana na upungufu wa lishe duniani. Na kutokufanya vizuri kwa watoto shuleni huweza kuwa dalili mojawapo. Kiasi cha nyama unachokitumia kwenye mlo kila siku kina faida kubwa ambayo huwezi kuifikiria. Kwa mujibu wa wataalamu wa afya, hata kiasi kidogo unachokula kwa kimeonyesha utofauti mkubwa kwenye uwezo wa mwili kufyonza madini ya chuma kutoka vyanzo mbalimbali.

Inafahamika kwamba wazazi wengi huwapatia watoto wao vyakula ambavyo ni muhimu kwenye ukuaji wao. Kama mzazi au mlezi jaribu aina mbalimbali ya vyakula mbali na vilivyoorodheshwa humu, fuata ushauri wa wataalamu mbalimbali wa afya au kusoma zaidi majarida tofauti ya afya na lishe.  

Post a Comment

0 Comments