Ushirikishwaji wananchi waokoa uharibifu hifadhi ya mazingira asili ya chome

 Wananchi wa vijiji vinavyoizunguka hifadhi ya mazingira asili ya Chome iliyopo wilayani Same mkoani Kilimanjaro wamekuwa washirika wakubwa katika uhifadhi baada ya kupatiwa shughuli mbalimbali mbadala rafiki na mazingira ambazo mbali na  kujipatia kipato zimewapunguzia kasi ya kuingia ndani ya hifadhi na kuvuna rasilimali za misitu zikiwemo kuni,mbao na uchomaji mkaa kwa ajili ya kujipatoa mahitaji.
Mfuko wa Uhifadhi wa milima ya Tao la mashariki(EAMCEF)ndio waliowajangea uwezo wananchi hao baada ya kujiunga kwenye vikundi vya uzalishaji .

Miongoni mwa vijiji vilivyonufaika na mpango huo ni kijiji cha Ndolwa kilichopo katika kata ya Vudee ambacho kikundi cha wafugaji nyuki cha Mkombozi kilipatiwa jumla ya mizinga 60 ya kisasa na vifaa vya kurinia asali yakiwemo mavazi na mashine ya kucakata asali.

Kwa mujibu Mwenyekiti wa kikundi hicho Ntarishwa Mnzava kwa kuvuna asali iliyotokana na mizinga hiyo wamefanikiwa kupanua mradi wao kwa kuuza asali na kununua mizinga mingine na kwa sasa wana jumla ya mizinga 100.
"pamoja na kuongeza idadi ya mizinga lakini pia tumekuwa tukigawana fedha zinazotokana  na mapato ya asali ambazo zimekuwa msaada mkubwa sana kwetu kwenye kuwapeleka watoto shule na mahitaji mengine ya familia lakini baadhi yetu wameweza kununua mifugo kama kuku na mbuzi ambao wameongeza mnyororo wa kipato cha familia"alisema Mnzava na kuongeza kuwa kwa msimu wamekuwa wakivuna asali mpaka zaidi ya lita 400.

Akizungumzia jitihada hizo zinazofanywa na EAMCEF kuwashirikisha wananchi katika utunzaji wa mazingira ya hifadhi ya Chome Afisa mtendaji wa kijiji hicho cha Ndolwa Yassir Ayoub alisema mradi huo wa ufugaji nyuki umesaidia pia katika urejeshaji wa uoto wa asili vikiwemo vyanzo vya maji vilivyokuwa vimekauka kutokana na ukataji wa miti lakini mizinga inayotundikwa msituni imekuwa ni nia mojawapo ya ulinzi,ambapo alieleza pia kuwa kutokana na kipato wanachopata wanakikundi kimesaida hata kwa upande wa elimu kwa watoto kupatiwa mahitaji yao ya msingi na kupunguza utoro.

Pamoja na ufugaji wa nyuki na miradi mingine ikiwemo ya ujenzi wa majiko banifu na ufugaji wa samaki , EAMCEF pia inatekeleza mpango wa kuzijenge uwezo kamati za mazingira za vijiji zilizoundwa kisheria ili kudumisha doria ndani ya hifadhi kwa kuzipatia mafunzo ya ulinzi shirikishi,kuwapatia sare za ulinzi pamoja na vitendea kazi vingine,mingoni mwa vijiji vilivonufaika na mpango huo kikiwa ni Kijiji cha Mhero kilichopo katika ya Chome.

Mwenyekiti wa kijiji hicho cha Mhero Thomas Fue alieleza kuwa kwa wanakamati kupatiwa mafunzo pamoja na sare imewajengea kutambulika wanapofanya kazi zao za ulinzi hifadhini ambapo kwa asilimia kunwa wamefanikisha kudhibiti uharibu uliokuwa ukifanywa na baadhi ya wananchi kuingiza mifugo hifadhini na wengine kuvuna mbao ndani ya msitu.

Kwa upande wa uongozi wa Hifadhi ya Mazingira asili ya Chome mwakilishi wa hifadhi hiyo Samweli Mtaning'ombe anakiri kuwepo kwa mabadiliko chanya ndani ya msitu baada ya wananchi kujengewa uwezo wa kujipatia kipato mbadala na kuimarishwa doria ambapo alieleza kuwa kutoakana na uhaba wa watumishi awali ilikuwa ni ngumu kumudu kudhibiti uhalifu ndani ya hifadhi lakini kwa sasa wananchi wenyewe wamekuwa walinzi baada ya kutambua umuhimu wa hifadhi hiyo kwa uendelevu wa maisha yao.

Afisa miradi wa EAMCEF kanda ya kaskazini Magreth Victor alisema mfuko huo umekuwa ukitoa ruzuku kwa Hifadhi ya mazingira asili ya Chome kila mwaka zaidi ya Shilingi milioni 25 kwa ajili ya kuboresha miundombinu ya hifadhi ikiwemo usafishaji wa mipaka pamoja na kuongeza doria lakini pia kuwajengewa uwezo wananchi kwa kuwapatia shughuli mbadala ili wawe walinzi bora wa msitu kutokana na umuhimu wa milima hiyo ambayo ndiyo chanzo kikuu cha maji yanayotegemewa kwenye matumizi mbalimbali yakiwemo ya nyumbani,umwagiliaji na hata uzalishaji wa umeme katika bwawa la Nyumba ya Mungu.

Mkuu wa wilaya ya Same Rdward Mpogolo aliahidi serikali wilayani humo kuendelea kushirikiana na Mfuko wa Uhifadhi wa Milima ya Tao la Mashariki EAMCEF kwa uhifadhi endelevu wa hifadhi ya mazingira asili ya Chome ambapo alisema wako mbioni kufanya operesheni maalum ya kuwasaka wale wanaokwenda kinyume na sheria za uhifadhi kwa kuendelea kuendesha shughuli za binadamu ndani ya hifadhi.
"wadau wamekuwa wakijitoa kushirikiana na wananchi kuuhifadhi msitu wa chome lakini bado wapo wachache wanaojaribu kuendeleza uhalifu,niwatahadharishe tu kuwa operesheni itakayoanza haitakuwa na msamaha"alisema mpogolo.

Hifadhi ya mazingira asili ya Chome ina eneo lenye ukubwa wa hekta 14,283,ikiwa ndani ya kilele cha milima ya Upare na imesheheni vivutio mbalimbali ikiwemo miti mikubwa,ndege wa aina mbalimbali,maporomoko na maji,maeneo ya asili yaliyokuwa yakitumiwa na wazee wa kabila la Wapare kwa ajili ya mila ambavyo vyote vimekuwa vivutio vikubwa kwa watalii .

Post a Comment

unashauriwa kutoa maoni muda na wakati wowote na kama unahabari yeyote unaruhusiwa kututumia

Previous Post Next Post