NASARI AREJESHA FOMU YA UBUNGE ARUMERU MAGHARIBI, AWAHIDI WANANCHI MAENDELEO
NASARI AREJESHA FOMU YA UBUNGE ARUMERU MAGHARIBI, AWAHIDI WANANCHI MAENDELEO
Mgombea ubunge Jimbo la Arumeru Magharibi Joshua Nasari akirejesha fomu ya kugombea Jimbo hilo kwa tiketi ya CCM
Na Woinde Shizza , Arusha
Arumeru Magharibi leo iligeuka kuwa na shamrashamra za aina yake baada ya mgombea ubunge kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM), Joshua Nasari, kurejesha rasmi fomu ya kugombea katika Ofisi za Msimamizi wa Uchaguzi wilayani humo.
Wananchi kutoka vijiji na kata mbalimbali walifurika kwa wingi kumsindikiza, wakiwa na nyuso za furaha, nderemo na vifijo, wakionesha imani kubwa waliyonayo kwake ,barabara za kuelekea ofisini hapo zilipambwa na mavazi ya kijani na njano, huku wananchi wakibeba mabango yenye jumbe za matumaini na maendeleo ambapo mbali na hilo pia Katika kunogesha mgombea ubunge hiyo aliingia Katika ofisi za chama na usafiri wa helkopta
Akizungumza mara baada ya kurejesha fomu, Nasari alisema safari ya maendeleo ya Arumeru Magharibi imefika katika hatua mpya na kwamba yeye yupo tayari kusimama bega kwa bega na wananchi kushughulikia changamoto zinazowakabili kwa muda mrefu.
“Changamoto za maji, barabara na huduma nyingine muhimu lazima zipate ufumbuzi, huu ni wakati wa kuibadilisha Arumeru na kuifanya wilaya yenye matumaini mapya, Nitashirikiana na wananchi na viongozi wote kuhakikisha kila mmoja anafaidika na matunda ya maendeleo,” alisema Nasari kwa msisitizo.
Aliwataka pia madiwani wa chama hicho kufanya kazi kwa makini na kwa bidii, akisisitiza kuwa maendeleo ya wananchi yanahitaji mshikamano na mshirikiano wa pamoja.
“Nitakuwa mbunge wa vitendo, siyo wa posho ,nitasimama mstari wa mbele kushirikiana na viongozi wenzangu kuwaletea maendeleo, kwa sababu wananchi wa Arumeru wanahitaji vitendo na si maneno matupu,” alisema huku akishangiliwa na wananchi.
Aidha Nasari aliwaomba wananchi kujitokeza kwa wingi siku ya kupiga kura ili kumpa kura Rais, mbunge na madiwani kupitia CCM, huku alibainisha kuwa ni chama pekee kinachoweka mbele maendeleo ya Watanzania.
Aliwashukuru wananchi wote waliomsindikiza na kumuunga mkono, akiahidi kuwalipa imani hiyo kwa kushirikiana nao kuhakikisha ndoto ya maendeleo inatimia kwa kila kijiji na kila kaya.





0 Comments:
إرسال تعليق
unashauriwa kutoa maoni muda na wakati wowote na kama unahabari yeyote unaruhusiwa kututumia