SEED CO WAHAMASISHA WAKULIMA KUACHANA NA KILIMO CHA MAZEOEA
Na Woinde Shizza , Arusha
Kampuni ya mbegu ya Seed Co imewataka wakulima kuachana na kilimo cha mazoea na badala yake kufuata kanuni, sheria na ushauri wa kitaalamu ili kuongeza tija na kuvuna mazao yenye ubora.
Wakizungumza kwenye banda lao katika maonyesho 31 ya Nanenane 2025 yanayoendelea Kanda ya Kaskazini, jijini Arusha, ofisa kilimo kutoka kampuni hiyo Peter Timoteo alisema changamoto kubwa inayowakabili wakulima wengi ni kuendelea kutumia mbegu zisizo na ubora na mbinu za kilimo zisizo na tija.
“Wakulima wengi bado wanalima kwa mazoea, bila kuzingatia kanuni za kitaalamu, tunawaambia, kilimo siyo kubahatisha ,hivyo ni lazima uchague mbegu bora, uzingatie ratiba ya kupanda, mbolea sahihi na kudhibiti magonjwa kwa wakati,” alisema mmoja wa maofisa wa kampuni hiyo.
Aidha baadhi ya wakulima waliotembelea banda hilo walisema elimu hiyo imewafungua macho “Tulizoea kutumia mbegu tulizobakiza msimu uliopita, lakini sasa tumejua hatari zake na faida za mbegu bora,” alisema Mary Mollel, mkulima kutoka Monduli.
Maonyesho ya Nanenane yameendelea kuwa chachu ya kuwaleta pamoja wakulima, watafiti na wadau wa sekta ya kilimo ili kujenga taifa linalojitegemea kwa chakula na kuongeza kipato cha wananchi kupitia kilimo chenye tija.

0 Comments:
إرسال تعليق
unashauriwa kutoa maoni muda na wakati wowote na kama unahabari yeyote unaruhusiwa kututumia