EACJ YATIMIZA MIAKA 10 TANGU KUZINDULIWA


MAHAKAMA ya Haki ya Afrika Mashariki, (EACJ) imetimiza miaka 10 tangu ilipozinduliwa na kuanza kazi Novemba 2001, ikijivunia kujenga misingi na kanuni licha ya kuwepo kwa changamoto kadhaa mbele yake. SIKIA MANENO ya  Msajili wa mahakama hiyo, Dk. John Luhangisa, kama ifuatavyo.


Swali: Mahakama yako ina umri wa miaka 10 sasa, je, unaridhika na utendaji wake?

Jibu: Binafsi ninaridhika na utendaji wa mahakam hii pamoja na majaji na wafanyakazi wake. Majaji na wafanyakazi wana moyo wa kujituma na hii inajionyesha kwa jinsi wanavyofanyakazi hadi zaidi ya muda uliopangwa. Mathalan, wengi hufanya kazi hadi saa 2 za usiku ingawa muda rasmi wa kumaliza kazi ni saa 11 jioni. Majaji wakija hapa hawana siku za sikukuu au Jumapili, wanachapa kazi muda wote.

Swali: Hii mahakama ina wafanyakazi na majaji wangapi na wanapataje nafasi hiyo?

Jibu: Mahakama inao majaji 10, na wote huteuliwa na Mkutano wa Wakuu wa nchi tano husika. Wafanyakazi wengine wapo 20 ambao walipata nafasi zao baada ya kutuma maombi ya kazi.

Swali: Mahakama hii ina tofauti gani na mahakama zingine?

Jibu: EACJ inasikiliza kesi za madai tu, tofauti na mahakama zingine ambazo husikiliza pia kesi za jinai. Pili, mtu ye yote akihitaji kufungua kesi hapa, hahitaji kwanza kupata kibali sehemu yo yote. Na tena mtu ye yote anaweza kufungua kesi dhidi ya nchi nyingine mwanachama kama imekiuka makubaliano yake (mkataba wa Jumuiya), basi anawza kufungua kesi dhidi ya nchi hiyo. Kwa mfano, shirika moja lisilo la kiserikali la Kenya, Africa Network for Animal Welfare (ANAW) limefungua kesi dhidi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali ya Muungano ya Tanzania, likipinga azma yake ya kujenga barabara kupita Mbuga ya Wanyamapori ya Serengeti kwa maelezo kuwa azma hiyo ni uvunjifu wa sheria na ni ukiukwaji wa kanuni za Mkataba wa Jumuiya ya Afrika Mashariki

Swali:  Baada ya uhai wa miaka 10 ya mahakama yako, imepata mafanikio gani?

Jibu: Mafanikio yamekuwa mengi. Kwanza imeweza kujenga misingi ambayo walalamikaji au mtu ye yote yule ambaye angependa kuleta kesi yake mahakamani hapa ataitumia. Yaani, mahakama imetengeneza kanuni za uendeshaji wa kesi za hapa na hii ni dira muhimu sana.

Pia imesimama kama taasisi inayojitegemea na yenye kutoa haki bila woga wala upendeleo, mfano halisi ni maamuzi ya kesi zilizofanywa imeonyesha kuwa ni taasisi ambayo imejijenga kuwahudumia watu bila woga na chuki.

Misingi mingine ni uwezo wa kutumiwa na mtu ye yote yule na hii unakuta katika kanuni zake ambazo hutoa nafasi kwa mtu ye yote bila kujali uwezo wake kufungua kesi katika mahakama hii. Na kwa upande wa mtu asiye na uwezo, mahakama inatoa nafasi kwa mtu huyo baada ya kujiridhisha kwamba ni kweli hana uwezo, kufungua kesi bila kutozwa gharama. Gharama ya kufungua kesi ni dola za Marekani 500 au chini ya hapo.

Swali: Unaweza kueleza changamoto ambazo inakabiliwa nazo?

Jibu: Kuna tatizo la uhaba wa majaji wa kusikiliza kesi. Majaji wanaosikiliza kesi katika mahakama hii hawakai hapa makao makuu ya EACJ Arusha, bali katika nchi zao husika. Wanakuja pale hitaji linapotokea, hivyo ni ngumu kuwapangia kazi za hapa. Sasa Baraza la Mawaziri linatakiwa kuamua majaji wakae hapa muda wote na hiyo inaweza kuendesha kesi na kumaliza kwa wakati muafaka. Suala la wafanyakazi pia ni tatizo kwani hawapo wa kutosha kulingana na kazi zilizopo.

Swali: Kuna uwezekano wa EACJ kupanua wigo wa utendaji kazi zake?

Jibu: Kuongeza wigo ni suala la wananchi wenyewe, wote wanataka wigo wa mahakama hii upanuliwe, yaani, iwe ya rufaa. Iweze pia kusikiliza kesi zinazotoka mahakama kuu au mahakama za rufani za nchi husika. Huo ndio wito wao na hayo ndiyo maoni ya wananchi.
Bahati nzuri kwa mujibu wa mkataba, EACJ baadaye itakuwa na uwezo wa kusikiliza kesi za rufaa.

Pia EACJ itakuwa na madaraka ya kusikiliza kesi zinazohusu haki ya binadamu, lakini mpaka sasa mkataba haujatengenezwa. Kwa sasa Mahakama ya Haki za Binadamu ya Afrika ndiyo yenye madaraka hayo.

Swali: Ni kesi ngapi hadi sasa zimekwishamuliwa na zilikuwa zinahusu nini hasa?

Jibu: Kwa mara ya kwanza mahakama ilipokea kesi Desemba 2005, iliyofunguliwa na wajumbe wa Bunge la Afrika Mashariki (EALA) kuhusu uchaguzi wa wabunge wa bunge hilo. Kesi hii ilikuwa ya Kenya, ambapo waliofungua walipiga uteuzi wa wabunge katika bunge hilo badala ya kuchaguliwa. Kesi nyingine ilifunguliwa mwaka 2006. 
Kuanzia hapo, mahakama ilipokea kesi tatu mwaka 2007, kesi moja mwaka 2008 na moja mwaka 2009 ambazo zilisikilizwa na kuamuliwa. Mwaka 2010 mahakama ilipokea kesi tisa ambazo bado zinasikilizwa, na mwaka huu, mahakama imepokea kesi tano.
Kesi zinazofunguliwa ni za madai kama uchaguzi, gharama za kesi, unyanyasaji, fidia ya uchelewezaji wa bidhaa kama bandarini, katiba na pensheni.


Swali: Miaka 10 ya uhai wa EACJ ni mingi, lakini kitu cha ajabu bado haifahaki sana kwa wananchi, unasemaje kuhusu hilo na kama kuna mikakati yo yote ya makusudi kuifanya ifahamike zaidi?

Jibu: Hiyo ni moja ya changamoto kwetu. Haifahamiki kiasi cha kutosha lakini tumedhamiria kujitangaza sana. Tunataka kuvitumia vyombo vya habari katika kuteleza matakwa hayo, kama vile televisheni, radio, magazeti na majarida. Tutakuwa tunarekodi vipindi na kuvipeleka katika vituo vya televisheni au radio kwa manufaa ya wananchi ili waweze kuifahamu mahakama yao na shughuli inazofanya.

Njia nyingine tunayoituma kujitangaza kwa wananchi ni kufanya mikutano na  makongamano na tumekwishazungumza na wanasheria wote wa nchi tano husika na kongamano la mwisho litafanyika Nairobi, Kenya, Juni 28 na 29 mwaka huu.

Mkakati mwingine wa kuhakikisha kwamba mahakama hii inafahamika zaidi ni uamuzi wa kufanya vikao vya mahakama kwa nchi wanachama. Hatua hii naona itasaidia kufanya watu waifahamu zaidi mahakama yao.

Swali: Bajeti ya EACJ ni kiasi gani na inatosheleza mahitaji?

Jibu: Bajeti yetu ni dola za Marekani 2,280,000. Hazitoshelezi bali tunajikita katika vipaumbele zaidi kama ilivyoanishwa katika Mpango Mkakati wa 2010-2015.

Post a Comment

unashauriwa kutoa maoni muda na wakati wowote na kama unahabari yeyote unaruhusiwa kututumia

Previous Post Next Post