TUSIPOKUWA WAANGALIFU MADINI ,GESI VITAKUWA LAANA


                                       


MHADHIRI mwandamizi kutoka Chuo Kikuu cha Mzumbe, Shule ya Dar es Salaam, Dk. Honest Ngowi, ameitahadharisha serikali kujenga misingi mizuri ya kunufaika na raslimali za madini na gesi kwa kujifunza kutoka nchi zingine za Afrika ambazo raslimali hizo zimegeuka kuwa laana badala ya kujenga uchumi wa nchi zao na wananchi kwa ujumla.

Akitoa mifano ya nchi za Afrika (majina yanahifadhiwa) zenye madini, gesi na mafuta,  Dk. Ngowi alisema hakuna ambayo imeonekana kunufaika na raslimali hizo,  huku wananchi wake wakiendelea kuogelea katika lindi la umaskini.

Dk.  Ngowi alitoa tahadhari hiyo kufuatia kugundulika kwa madini mengi ya uranium na gesi nchini, lakini akaonyesha wasiwasi wake iwapo raslimali hizo kama zimewekewa mfumo mzuri wa kunufaisha taifa na wananchi wake.

Alikuwa akizungumza kwenye mafunzo ya siku moja yanayoandaliwa na Shirika la Hakikazi Catalyst la jijini Arusha ya kuwajengea uwezo wananchi na viongozi wa kata, vijiji na vitongoji kutoka mikoa ya Tanga, Kilimanjaro, Arusha na Manyara, kuhusu kupanda kwa gharama za maisha na umaskini Tanzania:  Serikali inafanya jitihada gani na wananchi wanashiriki vipi?
“Bila kuweka mfumo mzuri wa mkunufaisha mwananchi,  madini, gesi na baadaye mafuta, yatakuwa ni laana kwao…watakaonufaika sio  wananchi bali mataifa yaliyoendelea,” alisema.

Alisema baadhi ya nchi zenye kuzalisha mafuta mengi na mazuri duniani,  hazijaendelea kiuchumi kutokana na kukosa mfumo sahihi wa kunufaika na mafuta hayo.

Kuhusu kupanda kwa bei ya mafuta, hususan, mikoani, Dk. Ngowi alipendekeza kujengwa kwa bomba la mafuta kutoka Dar es Salaam hadi Mwanza ili kuwarahisha upatikanaji wake katika mikoa ya Kanda ya Ziwa.

Hata hivyo, mikakati ya ujenzi wa bomba hilo ulianza tangu wakati wa awamu ya tatu ya Rais Ben Mkapa hadi miaka ya mwanzoni ya awamu ya nne ya Rais Jakaya Kikwete, na mpaka sasa hakuna taarifa zo zote zilizotolewa na serikali kuhusu kuendelea na ujenzi huo au la.





Post a Comment

unashauriwa kutoa maoni muda na wakati wowote na kama unahabari yeyote unaruhusiwa kututumia

Previous Post Next Post