MCHUNGAJI UWINKINDI AKATAA KUJIBU MASWALI YA MWENDESHA MASHITAKA

Mshitakiwa wa mauaji ya kimbari ya Rwanda, Jean Uwinkindi, amekataa kwa mara ya nne mfululizo kujibu maswali ya mwendesha mashitaka wa Mahakama Kuu ya Kigali, nchini Rwanda alikopelekwa kusikilizwa maelezo ya awali ya kesi inayomkabili.
Kwa mujibu wa Msemaji wa Mwendesha Mashitaka, Alain Mukurarinda, Uwinkindi anadai kwamba ‘’ana haki ya kukaa kimya.’’ 
Mchungaji Uwinkindi alitiwa mbaroni Juni 30, 2010 nchini Uganda na kuhamishiwa makao makuu ya ICTR, mjini Arusha, Tanzania, siku mbili baadaye.Aprili 19, 2012 akawa mshitakiwa wa kwanza wa ICTR, kesi yake kuhamishiwa nchini Rwanda kwenda kusikilizwa katika Mahakama Kuu ya nchi hiyo. Alikana tuhuma zote dhidi yake. 
Kukataa kwake kuzungumza hakuzuii kesi kuendelea kusikilizwa, Mukurarinda aliliambia Shirika la Habari la Hirondelle. ‘’Usikilizaji wa awali wa kesi hiyo unatarajiwa kuanza kama ilivyopangwa Agosti 27, 2012.’’ 
Gatete Gashabana, Wakili wa utetezi wa Uwinkindi hakutaka kusema lolote kuhusiana na kukataa kwa mteja wake kujibu maswali ya mwendesha mashitaka, lakini aliliambai Shirika la Habari la Hirondelle kwa njia ya simu kwamba wako tayari kwa kusikiliza maelezo ya awali. ‘’Tutaomba mteja wetu aachiwe kwa dhamana,’’ aliongeza. 
Mchungaji Uwinkindi anashitakiwa kwa mauaji ya kimbari na kuteketeza kizazi. 

Post a Comment

unashauriwa kutoa maoni muda na wakati wowote na kama unahabari yeyote unaruhusiwa kututumia

Previous Post Next Post