Afisa Kilimo Karatu: Wakulima Wafate Ushauri wa Wataalamu kwa Mazao Bora na Salama
Na Woinde Shizza, Arusha
Afisa Kilimo na Mifugo wa Halmashauri ya Wilaya ya Karatu, Wayda Sulle, amewataka wakulima wilayani humo kuhakikisha wanashirikiana kwa karibu na wataalamu wa kilimo waliopo katika maeneo yao, kwa lengo la kupata elimu sahihi itakayowasaidia kuongeza uzalishaji na tija katika shughuli zao.
Akizungumza kwenye maonyesho ya wakulima ya 31 yanayofanyika Katika viwanja vya njiro nane nane Sulle alisema kuwa baadhi ya wakulima wamekuwa wakipata hasara kutokana na kutofuatilia ushauri wa kitaalamu na kutegemea mbinu za kilimo za mazoea.
“Tuna wataalamu waliopo kwenye vijiji vyetu, ni muhimu sana wakulima wetu wawe karibu nao, waulize maswali, wapate elimu bora ya kilimo hii ndiyo njia sahihi ya kupata mazao mengi yenye tija,” alisema Sulle.
Alihimiza matumizi ya mbolea asilia zisizo na kemikali, akibainisha kuwa ni salama kwa afya ya binadamu na mazingira, na pia zinasaidia kulinda viumbe hai wa udongo kama minyoo na bakteria, ambao huchangia kuchakata virutubisho vinavyohitajika na mimea.
“Mbolea za asili husaidia mimea kukua vizuri, lakini pia zinaongeza usalama wa chakula chetu ,” alisisitiza.
Moja ya Mkulima aliejitambulisha kwa Jina la Adili Msangi kutoka Karatu alisema kuwa elimu aliyoipata imemfungua macho kuhusu umuhimu wa kushirikiana na maafisa ugani na matumizi ya mbolea salama.
“Nimekuwa nikitumia mbolea za kemikali bila kuelewa madhara yake ,leo nimejifunza kuwa kuna njia mbadala, bora na salama zaidi Nipo tayari kubadilika,” alisema Msangi.
Aidha aliwataka wakulima kuacha kutegemea uzoefu wa zamani pekee katika kilimo na badala yake waendelee kujifunza kutoka kwa wataalamu ili kulima kwa tija, kulinda afya na kuchangia uchumi wa familia na taifa kwa ujumla.


0 Comments:
Post a Comment
unashauriwa kutoa maoni muda na wakati wowote na kama unahabari yeyote unaruhusiwa kututumia