Ticker

6/recent/ticker-posts

BILIONI 200 ZA MIKOPO ZIMETOLEWA NA TPB KWA WANAJESHI WASTAAFU


Na Woinde Shizza ,ARUSHA.
Benki ya Posta ( TPB) imetoa mikopo yenye thamani ya shilingi Bilioni 200 kwa Wanajeshi Wastaafu wa   Jeshi la JWTZ nchini  ili waweze kujiendeleza kiuchumi na kuboresha maisha yao baada ya kustaafu .
Mkurugenzi wa Mikopo wa Benki hiyo Henry Jonathan amesema kuwa wametoa mikopo hiyo kwa kipindi cha miaka mitatu tangu waanze kutoa mikopo kwani benki hiyo inaongoza kwa kutoa mikopo mingi kwa wastaafu ambayo inawasaidia kuinua hali ya maisha na kuanzisha miradi ya uzalishaji.
Kwa  Mkoa wa Arusha wenye jumla ya wastaafu 600 wametoa bilioni 13.7  za mikopo kwa wastaafu hao ambao ni wanufaika wakubwa wa fursa hiyo ya mikopo.
“Kama unavyojua benki ya posta inaongoza kwa kutoa mikopo kwa wastaafu ili kuboresha maisha yao na kuhamasisha uwekezaji wenye tija utakaoinua vipato vyao na jamii kwa ujumla” Alisema Mkurugenzi huyo
Mwenyekiti wa Umoja wa Wanajeshi wastaafu unaofahamika kama MUWATA, Luteni Mstaafu  Geofrey  Wapalila amesema kuwa mikopo hiyo imewasaidia kufungua biashara na kuwa wajasiriamali hasa wanapoanza maisha uraiani hivyo kuendeleza maisha yao vizuri pia wameishukuru benki hiyo kwa kuwaamini.

Pia ameiomba benki hiyo kutoa mikopo ya vifaa kwa wajasiriamali ili waweze kuzalisha kwani bado wana nguvu za kufanya shughuli za uzalishaji.
Mmoja wa Wastaafu hao  Leonard Kilasi ameshauri wastaafu hao kukopa kwa busara na kulipa kwa wakati ili mikopo hiyo iwe na tija na kusaidia maisha yao.

Post a Comment

0 Comments