WAFANYABIASHARA wa madini mkoani Arusha, wameiomba Kampuni ya
Magazeti ya Serikali (TSN) iandae Jukwaa la Fursa la Kibiashara la
tanzanite, kuzungumzia changamoto zinazowakabili.
Wamesema sekta ya madini ni moja ya sekta kubwa nchini, inayoinua
uchumi wa nchi. Lakini, walisema sekta hiyo ina changamoto kubwa
zinazopaswa kutatuliwa.
Mmoja wa wafanyabiashara wa madini ya tanzanite, Japhet Shoo, alisifu jitihada za jukwaa hilo.
Alisema ni lazima serikali ijiulize ni kwa nini bado mpaka sasa haijanufaika na madini ya tanzanite.
Amesema jambo kubwa linalowasumbua wamiliki na wachimbaji wa madini
ni upatikanaji wa zana za uchimbaji, kwani shughuli hiyo inapaswa
kufanywa na wafanyabiashara wengi na kwa bei poa. Aliomba serikali
kuondoa kodi ya uingizaji wa zana za uchimbaji.
Changamoto nyingine inayowakabili wamiliki wa migodi ni zana za uchimbaji, kwa kuwa zinauzwa na watu wachache.
Naye Julius Laizer anayechimba madini ya tanzanite, amesema uongozi
wa juu wa TSN unapaswa kupongezwa kwa kuwa wabunifu na kuwahamasisha
wafanyabiashara, kueleza kero zao kupitia magazeti yao na kisha
kuyafanyia kazi kwa kuwauliza watendaji wa serikali na kupata majibu
sahihi ya kero hizo.
Laizer alisema watendaji wa serikali, wamezidiwa na majukumu ya kila
siku, hivyo wamesaidiwa kwa namna moja ama nyingine na Jukwaa la Fursa
ya Biashara, linaloandaliwa na kampuni hiyo ili kila mfanyabiashara
afanye kazi kwa uwazi na uhuru bila ya kuwa na migongano.
Alisema wachimbaji na wauzaji wa madini nchini, wana changamoto
nyingi, ambazo zinatakiwa kupatiwa majibu sahihi ili sekta hiyo iweze
kuendelea kwa faida ya uchumi wa nchi yetu.
Mfanyabiashara huyo alisema mahali pekee panapotakiwa wao kutoa dukuduku zao ni Jukwaa la Biashara la TSN.
Alisema angependa siku hiyo Waziri wa Madini, Katibu Mkuu wa Wizara
ya Madini na Kamishna wa Madini wawepo ili changamoto zao ziweze kupata
majibu.
Mfanyabiashara mwingine, Hassan Juma, muuzaji na mnunuzi wa madini
alisema wafanyabiashara wa madini mkoani Arusha, hawakualikwa katika
jukwaa hilo.
Aliusifu uongozi wa TSN kwa kubuni mbinu ya kukutana na
wafanyabishara na kueleza kero zao na kuzianika katika magazeti ya
serikali na kwa muda mfupi zinapatiwa majibu sahihi na kwa wakati.
Juma alisema kuwa kipindi kijacho, jukwaa hilo linapaswa kutoa
kipaumbele kwa sekta ya madini, kwa kuwakutanisha wafanyabiashara wote
wa mkoa wa Arusha na wamiliki wa migodi, ili kila mmoja aweze kusema
matatizo yanayomkabili.
-
0 Comments
unashauriwa kutoa maoni muda na wakati wowote na kama unahabari yeyote unaruhusiwa kututumia