Ticker

6/recent/ticker-posts

AHADI YA KURUDISHA UTULIVU KATIKA TARAFA YA MANYARA YAANZA KUTEKELEZWA





Ikiwa ni siku 11 tu kupita toka Kamanda wa Polisi mkoa wa Arusha (SACP) Ramadhani Ng’anzi kuahidi kurudisha utulivu katika tarafa ya Manyara wilayani Monduli, kwa sasa eneo hilo limezidi kuimarika kiusalama baada ya kufanyika doria na operesheni za mara kwa mara na jana katika mkutano wa hadhara uliofanyika uwanja wa Barafu Mto wa Mbu alizindua vikundi Tisa vya ulinzi shirikishi vilivyokuwa na jumla ya askari 215.
Awali Kamanda Ng’anzi aliitoa ahadi hiyo alipokutana na viongozi wa Kata, Vijiji na Vitongoji katika kikao kilichofanyika ofisi ya Afisa tarafa tarehe 19 Julai mwaka huu ambapo viongozi hao walisema suala linalosababisha kuwepo kwa matukio ya uhalifu ni uhusiano hafifu baina ya baadhi ya askari Polisi, viongozi na wananchi hali ambayo inatoa mwanya kwa wahalifu kuendelea kufanya uhalifu.
Baada ya kuwasikiliza kwa umakini alibaini baadhi ya mambo ambayo yanayotakiwa yafanyike kwa haraka ikiwa ni pamoja na kufanya doria na operesheni usiku na mchana, askari Polisi kutoa huduma bora kwa wananchi hali ambayo itasaidia kuwa karibu nao na kupata taarifa za uhalifu lakini pia uanzishaji wa vikundi vya ulinzi shirikishi katika kila kitongoji ambapo aliwahakikishia viongozi hao kwa kusema kwamba eneo hilo litakuwa salama.
Kufuatia mikakati hiyo ya Kamanda Nga’nzi ambaye alisema yeye anapenda sana kutenda badala ya maneno mengi, siku hiyo hiyo aliongeza askari katika eneo hilo ambao walifanya operesheni katika maeneo tete, kwenye bar na nyumba za kulala wageni lakini pia alipiga marufuku kwa waendesha boda boda na Bajaji kufanya biashara hizo mpaka asubuhi.
Nao viongozi wa eneo hilo hawakuwa nyuma na kuamua kumuunga mkono kwa kuanzisha vikundi vya ulinzi shirikishi kama jinsi alivyoagiza, ambavyo vilipewa mafunzo toka kwa Maofisa toka Kitengo Polisi Jamii mkoa lakini pia kuahidi kutenga eneo na kujenga kituo kikubwa cha Polisi.
Katika mkutano huo uliohudhuriwa na umati mkubwa wa wakazi wa eneo hilo, aliwasitizia wananchi watoe ushirikiano wa kutosha kwa askari hao kwa kuwafichua wahalifu ili taarifa zao zifanyiwe kazi. 
Kamanda Ng’anzi alikiri kuwepo kwa upungufu wa askari Polisi na kusema kwamba uwepo wa vikundi hivyo vya Ulinzi Shirikishi utasaidia kupunguza pengo hilo huku akisisitiza uwepo wa amani utasaidia kukuza uchumi kwa wafanyabiashara wa eneo hilo ambao mara nyingi wanawahudumia watalii wanaokwenda na kurudi toka katika vivutio mbalimbali.
Kwa upande wake Kaimu Mkuu wa Chuo cha Mafunzo cha JKT Makuyuni Luteni Kanali Phesto Mbanga aliahidi kushirikiana na Jeshi la Polisi katika kuimarisha ulinzi eneo hilo la tarafa ya Manyara na kuwasisitiza wananchi nao wasibaki nyuma kwani suala la amani ni wajibu wa watu wote.
Awali akitoa taarifa juu ya mafunzo hayo kabla ya kumkaribisha Kamanda wa Polisi, Mkuu wa Kitengo cha Polisi Jamii mkoa wa Arusha Mrakibu Msaidizi wa Polisi (ASP) Edith Makweli alisema kwamba askari hao walifundishwa namna ya ukamataji salama,upekuzi, haki zao wanapokuwa kazini, silaha wanazotakiwa kutumia wakiwa kazini na Utii wa sheria bila shuruti.
Alisema mbali na mafunzo kwa askari hao lakini pia kwa kipindi cha wiki moja waliweza kutoa elimu kwa viongozi wa kata, vijiji na vitongoji juu ya wajibu wao, wamiliki wa nyumba za kulala wageni, Bar na Hoteli ambao wanatakiwa kuwa na leseni halali na kuhakikisha kwamba kumbi zao zipo salama. Aidha kwa upande wa madereva wa Bajaji na Boda boda walifundishwa mbinu za kupambana na uhalifu ikiwa ni pamoja na namna ya kutoa taarifa pamoja na sheria za usalama barabarani.







  Baadhi ya wananchi wa tarafa ya Manyara wilayani Monduli wakimsikiliza Kamanda wa Polisi mkoa wa Arusha (SACP) Ramadhani Ng'anzi wakati alipokuwa anaelezea mikakati iliyowekwa na Jeshi la Polisi ya kuzuia uhalifu katika eneo hilo.(Na Woinde Shizza,Arusha )




 Kamanda wa Polisi mkoa wa Arusha Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Polisi (SACP) Ramadhani Ng'anzi akiongea na wananchi wa Mto wa Mbu wilayani Monduli wakati wa mkutano wa uzinduzi wa vikundi Tisa vya ulinzi shirikishi vilivyokuwa na jumla ya askari 215. 
Kamanda wa Polisi mkoa wa Arusha Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Polisi (SACP) Ramadhani Ng'anzi pamoja na Kaimu Mkuu wa Chuo cha Mafunzo Cha JKT Makuyuni Luteni Kanali Phesto Mbanga wakiungana na wahitimu wa mafunzo ya Ulinzi Shirikishi kimba nyimbo za hamasa baada ya uzinduzi wa vikundi hivyo..

Post a Comment

0 Comments