Jeshi la Polisi
mkoani hapa kwa kushirikiana na Chuo cha Ufundi Stadi (VETA) kanda ya Kaskazini
wamefanikiwa kutoa mafunzo kwa madereva 350 wa magari ya abiria ambao awali
walikuwa na Leseni pekee bila vyeti.
Mafunzo hayo yaliyofungwa
na Mkuu wa Mkoa wa Arusha Bw. Mrisho Gambo katika Chuo Cha Ufundi Arusha, awali
yalifunguliwa na Kamanda wa Polisi mkoa wa Arusha Kamishna Msaidizi Mwandamizi
wa Polisi (SACP) Ramadhani Ng’anzi wiki mbili zilizopita.
Akizungumza katika
siku hiyo ya Mahafali, Mkuu huyo wa mkoa, kwanza kabisa alilipongeza Jeshi la
Polisi na Chuo cha Ufundi Stadi (VETA) kwa kuamua kuendesha mafunzo hayo lakini
pia kwa wahitimu wenyewe kwani ni jambo zuri na lenye maslahi kwenye maisha
yao.
Alisema jitihada
hizo zinalenga kupambana na ajali kwani madhara yake ni makubwa ikiwa ni pamoja
na kusababisha vifo, ulemavu, kupata hasara kwenye mali lakini pia zinaweza
kusababisha kutotoa fursa za ajira kwa madereva wenye matukio ya kusababisha
ajali.
Mkuu huyo wa mkoa alisema
pamoja na mafunzo waliyoyapata wahitimu hao lakini watatakiwa waepuke unywaji
wa pombe wakati wanaendesha vyombo vya moto kwani ajali nyingi zinasababishwa
na ulevi, huku akilitaka Jeshi la Polisi kupitia kitengo cha usalama Barabarani
kuongeza jitihada katika kupima ulevi kwa madereva.
“Pamoja na Mafunzo
mliyoyapata kuwajengea uwezo lakini kama hamtaepuka unywaji wa pombe wakati
mnaendesha vyombo vya moto ajali zitaendelea kutokea”. Alionya Bw. Gambo
Aliwataka Madereva
hao kuwa na nyaraka zote na vifaa vyote muhimu kama Vizima Moto pindi
wanapokuwa kazini na kusema ukamilifu wa vitu hivyo vitasaidia kuepusha mabishano
na askari wa Usalama barabarani.
Kwa upande wake
Kamanda wa Polisi mkoa wa Arusha Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Polisi (SACP)
Ramadhani Ng’anzi alisema anaamini mafunzo hayo yamewajengea uwezo na kuwapa
umahiri wa kuendesha magari ya abiria.
Alisema mafunzo hayo
yatasaidia mkoa wa Arusha kuwa ni miongoni mwa mikoa salama kwa kuepuka ajali
mbaya na kuahidi kuendeleza na kuzidi kuimarisha ushikiano kati ya Jeshi hilo
na Chuo cha Ufundi Stadi (VETA) ili mwisho wa siku Madereva wote wapate mafunzo
hayo.
Naye Mkuu wa Kikosi
cha Usalama Barabarani mkoa wa Arusha Mrakibu wa Polisi (SP) Joseph Charles
Bukombe alisema kwamba, wahitimu hao watakuwa Mabalozi wa wenzao na kuonya
kwamba wale wote ambao wanatengeneza na wanaonunua vyeti vya VETA bila kupata
mafunzo watakamatwa na kufunguliwa Mashtaka.
Awali akimkaribisha
Mgeni rasmi, Mkurugenzi wa VETA Kanda ya Kaskazini Bw. Anjelus Ngonyani alisema
kwamba ajali nyingi zinasababishwa na makosa ya kibinadamu ambayo yanatokana na
kukosa mafunzo. Alisema Chuo hicho kinatoa mafunzo bora na yanayokidhi viwango
na kuwataka madereva wazidi kujitokeza.
Mkuu wa Kikosi cha Usalama Barabarani mkoa wa Arusha Mrakibu wa
Polisi (SP) Joseph Charles Bukombe akiwataka Wahitimu hao wakawe
mabalozi wa madereva wengine ambao hawajapata mafunzo kama hayo ili nao
wajitokeze siku za usoni.
Baadhi ya wahitimu waliopata mafunzo ya uendeshaji wa magari ya
kubeba abiria ambayo yaliendeshwa na Chuo cha Ufundi Stadi (VETA) kwa
muda wa wiki mbili wakimsikiliza Mkuu wa mkoa wa Arusha Bw. Mrisho Gambo
wakati wa Mahafali hayo yaliyofanyika katika Chuo cha Ufundi Arusha.
0 Comments
unashauriwa kutoa maoni muda na wakati wowote na kama unahabari yeyote unaruhusiwa kututumia