Ticker

6/recent/ticker-posts

ARUSHA YAANZA KUONYESHA NJIA MADEREVA WASIOKUWA NA VYETI


Jeshi la Polisi mkoani hapa kwa kushirikiana na Chuo cha Ufundi Stadi (VETA) kanda ya Kaskazini wamefanikiwa kutoa mafunzo kwa madereva 350 wa magari ya abiria ambao awali walikuwa na Leseni pekee bila vyeti.
Mafunzo hayo yaliyofungwa na Mkuu wa Mkoa wa Arusha Bw. Mrisho Gambo katika Chuo Cha Ufundi Arusha, awali yalifunguliwa na Kamanda wa Polisi mkoa wa Arusha Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Polisi (SACP) Ramadhani Ng’anzi wiki mbili zilizopita.
Akizungumza katika siku hiyo ya Mahafali, Mkuu huyo wa mkoa, kwanza kabisa alilipongeza Jeshi la Polisi na Chuo cha Ufundi Stadi (VETA) kwa kuamua kuendesha mafunzo hayo lakini pia kwa wahitimu wenyewe kwani ni jambo zuri na lenye maslahi kwenye maisha yao.
Alisema jitihada hizo zinalenga kupambana na ajali kwani madhara yake ni makubwa ikiwa ni pamoja na kusababisha vifo, ulemavu, kupata hasara kwenye mali lakini pia zinaweza kusababisha kutotoa fursa za ajira kwa madereva wenye matukio ya kusababisha ajali.
Mkuu huyo wa mkoa alisema pamoja na mafunzo waliyoyapata wahitimu hao lakini watatakiwa waepuke unywaji wa pombe wakati wanaendesha vyombo vya moto kwani ajali nyingi zinasababishwa na ulevi, huku akilitaka Jeshi la Polisi kupitia kitengo cha usalama Barabarani kuongeza jitihada katika kupima ulevi kwa madereva.
“Pamoja na Mafunzo mliyoyapata kuwajengea uwezo lakini kama hamtaepuka unywaji wa pombe wakati mnaendesha vyombo vya moto ajali zitaendelea kutokea”. Alionya Bw. Gambo
Aliwataka Madereva hao kuwa na nyaraka zote na vifaa vyote muhimu kama Vizima Moto pindi wanapokuwa kazini na kusema ukamilifu wa vitu hivyo vitasaidia kuepusha mabishano na askari wa Usalama barabarani.
Kwa upande wake Kamanda wa Polisi mkoa wa Arusha Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Polisi (SACP) Ramadhani Ng’anzi alisema anaamini mafunzo hayo yamewajengea uwezo na kuwapa umahiri wa kuendesha magari ya abiria.
Alisema mafunzo hayo yatasaidia mkoa wa Arusha kuwa ni miongoni mwa mikoa salama kwa kuepuka ajali mbaya na kuahidi kuendeleza na kuzidi kuimarisha ushikiano kati ya Jeshi hilo na Chuo cha Ufundi Stadi (VETA) ili mwisho wa siku Madereva wote wapate mafunzo hayo.
Naye Mkuu wa Kikosi cha Usalama Barabarani mkoa wa Arusha Mrakibu wa Polisi (SP) Joseph Charles Bukombe alisema kwamba, wahitimu hao watakuwa Mabalozi wa wenzao na kuonya kwamba wale wote ambao wanatengeneza na wanaonunua vyeti vya VETA bila kupata mafunzo watakamatwa na kufunguliwa Mashtaka.

Awali akimkaribisha Mgeni rasmi, Mkurugenzi wa VETA Kanda ya Kaskazini Bw. Anjelus Ngonyani alisema kwamba ajali nyingi zinasababishwa na makosa ya kibinadamu ambayo yanatokana na kukosa mafunzo. Alisema Chuo hicho kinatoa mafunzo bora na yanayokidhi viwango na kuwataka madereva wazidi kujitokeza.

 Mkuu wa Mkoa wa Arusha Bw. Mrisho Gambo akiongea na Wahitimu wa mafunzo ya udereva wa magari ya abiria wakati wa Mahafali ya kuhitimisha mafunzo yao yaliyofanyika mwishoni mwa wiki katika ukumbi wa Chuo cha Ufundi Arusha

Mkuu wa Kikosi cha Usalama Barabarani mkoa wa Arusha Mrakibu wa Polisi (SP) Joseph Charles Bukombe akiwataka Wahitimu hao wakawe mabalozi wa madereva wengine ambao hawajapata mafunzo kama hayo ili nao wajitokeze siku za usoni.
 
Kamanda wa Polisi mkoa wa Arusha (SACP) Ramadhani Ng'anzi akitoa shukrani zake kwa Chuo cha Ufundi Stadi ( VETA) kwa kushirikiana na Jeshi la Polisi mkoani hapa katika kuendesha mafunzo ya muda mfupi kwa Madereva ambao hawana vyeti.


 

 Baadhi ya wahitimu waliopata mafunzo ya uendeshaji wa magari ya kubeba abiria ambayo yaliendeshwa na Chuo cha Ufundi Stadi (VETA) kwa muda wa wiki mbili wakimsikiliza Mkuu wa mkoa wa Arusha Bw. Mrisho Gambo wakati wa Mahafali hayo yaliyofanyika katika Chuo cha Ufundi Arusha.

Post a Comment

0 Comments