Ticker

6/recent/ticker-posts




Mgeni rasmi-Waziri wa kilimo Mhe. Dkt Charles Tizeba akizungumza wakati wa sherehe za ufunguzi wa masoko ya tumbaku Kitaifa iliyofanyika katika viwanja vya kata ya Mwendakulima Wilayani Kahama Mkoa wa Shinyanga, leo 12 Juni 2018. Picha Zote Na Mathias Canal, WK




Waziri wa kilimo Mhe. Dkt Charles Tizeba akimkabidhi cheti cha pongezi Mkulima Jonas Blakali kutoka Wilaya ya Bukombe Mkoani Geita ambaye ameshika nafasi ya tatu katika msimu wa kilimo cha tumbaku wa mwaka 2017/2018 wakati wa sherehe za ufunguzi wa masoko ya tumbaku Kitaifa iliyofanyika katika viwanja vya kata ya Mwendakulima Wilayani Kahama Mkoa wa Shinyanga, leo 12 Juni 2018.



Mgeni rasmi-Waziri wa kilimo Mhe. Dkt Charles Tizeba akikata utepew kuashiria ufunguzi wa masoko ya tumbaku Kitaifa katika sherehe iliyofanyika kwenye viwanja vya kata ya Mwendakulima Wilayani Kahama Mkoa wa Shinyanga, leo 12 Juni 2018.



Waziri wa kilimo Mhe. Dkt Charles Tizeba akisisitiza jambo wakati akishuhudia ununuzi wa tumbaku wakati wa sherehe za ufunguzi wa masoko ya tumbaku Kitaifa iliyofanyika katika viwanja vya kata ya Mwendakulima Wilayani Kahama Mkoa wa Shinyanga, leo 12 Juni 2018.



Baadhi ya wakulima wa tumbaku wakishuhudia sherehe za uzinduzi wa ufunguzi wa masoko ya tumbaku Kitaifa iliyofanyika katika viwanja vya kata ya Mwendakulima Wilayani Kahama Mkoa wa Shinyanga, leo 12 Juni 2018.



Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga Mhe Zainab Telack akizungumza kabla ya kumkaribisha mgeni rasmi ambaye ni Waziri wa kilimo Mhe. Dkt Charles Tizeba wakati wa sherehe za ufunguzi wa masoko ya tumbaku Kitaifa iliyofanyika katika viwanja vya kata ya Mwendakulima Wilayani Kahama Mkoa wa Shinyanga, leo 12 Juni 2018.

Na Mathias Canal, WK, Kahama-Shinyanga

Waziri wa kilimo Mhe Dkt Charles Tizeba amefungua masoko ya tumbaku Kitaifa huku akitoa onyo kali kwa wakulima waliolima zao hilo nje ya mfumo wa ushirika kwa mujibu wa sheria ya zao hilo kwa kuwataka kuacha mara moja kwani serikali itashughulika na wote wanaokiuka taratibu za kilimo hicho.

Dkt Tizeba ameyasema hayo leo 12 Juni 2018 katika viwanja vya kata ya Mwendakulima Wilayani Kahama Mkoa wa Shinyanga wakati akihutubia mamia ya wakulima wa tumbaku kwenye sherehe za ufunguzi wa masoko ya tumbaku Kitaifa.

Dkt Tizeba amemuagiza Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga Mhe Zainabu Telack kufanya kikao na Wakuu wa Wilaya na Wakurugenzi wa Wilaya zote za Mkoa huo kuhakikisha wanazuia wananchi kulima nje ya mfumo wa ushirika kwa mujibu ya sheria ya zao la tumbaku.

Alisema kuwa wigo wa soko la tumbaku unazidi kuwa finyu kutokana na viongozi mbalimbali kuwakumbatia baadhi ya wakulima wa tumbaku wanaolima nje ya mfumo wa zao hilo.

Katika sherehe hiyo Mhe Dkt. Tizeba amekabidhi vyeti vya pongezi kwa wakulima waliofanya vizuri katika msimu wa kilimo wa mwaka 2017/2018 ambao ni mkulima Emmanuel Cherehani kutoka Wilaya ya Ushetu aliyeshika nafasi ya kwanza, nafasi ya pili ni Jimson Mwanjwenga kutoka Wilaya ya Chunya Mkoani Mbeya na Jonas Blakali kutoka Wilaya ya Bukombe Mkoani Geita.

Awali akisoma risala kwa niaba ya wakulima wa zao la tumbaku Tanzania Kaimu Meneja Mkuu TCJE Ndg Bakari Kisia alisema kuwa zao la tumbaku limeanza kulimwa nchini Tanzania enzi za ukoloni kwa kuanzia mikoa ya Ruvuma (Tumbaku ya Moshi) na Iringa (Tumbaku ya mvuke) huku akisema kuwa umaarufu wa zao hilo umekuja mara baada ya masoko huria kuanzishwa.

Kisia amepongeza juhudi za serikali katika misimu miwili ya mwaka 2016/2017 na 2017/2018 kwa kutatua suala la kupanda kwa bei ya pembejeo huku akizitaja changamoto katika zao la tumbaku kuwa ni pamoja na kupungua kwa mahitaji ya tumbaku, Kushuka kwa bei ya wastani ya tumbaku, pamoja na Ukubwa wa riba za mikopo.

Akisoma taarifa ya maendeleo ya zao la tumbaku Tanzania Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Bodi ya tumbaku Tanzania Dkt Julius Ningu ameitaja mikoa inayolima tumbaku kwa wingi kuwa ni pamoja na Shinyanga, Kagera, Geita, Kigoma, Tabora, Rukwa, Mbeya, Morogoro, Iringa, Ruvuma na Mara huku akiutaja mkoa wa Tabora kuongoza kwa uzalishaji kwa takribani asilimia 50 ya tumbaku yote inayozalishwa nchini.

Alisema kuwa zao la tumbaku lina mchango mkubwa katika pato la Taifa ambapo pato la mkulima limeongezeka kutoka shilingi za kitanzania 2,242,030 mwaka 2011/2012 hadi shilingi 5,982,745 mwaka 2016/2017 ambapo ongezeko hilo ni sawa na asilimia 166.8

Makusanyo ya ushuru wa Halmashauri za Wilaya yameongezeka kutoka shilingi bilioni 10.8 mwaka 2011/2012 hadi shilingi bilioni 14.8 mwaka 2016/2017 ongezeko la asilimia 37. Huku mapato ya fedha za kigeni yakiwa yameongezeka kutoka dola milioni 302.8 mwaka 2011 hadi dola milioni 343.9 mwaka 2016/2017 ongezeko la asilimia 14

Post a Comment

0 Comments