SIMBU FOUNDATION YAZINDUA KAMPENI YA KUIBUA VIPAJI, SHIRIKISHO LA RIADHA LAUNGA MKONO JUHUDI HIZO
Na Woinde Shizza , Arusha
Mwanariadha wa kimataifa wa Tanzania, Alphonce Felix Simbu, kupitia Simbu Foundation, amezindua kampeni maalum ya mbio za hisani zinazolenga kuhamasisha ushiriki wa Watanzania katika michezo, kukuza vipaji vya vijana na kuchangia maendeleo ya mchezo wa riadha nchini.
Akizungumza wakati wa uzinduzi wa kampeni hiyo jijini Arusha, Simbu alisema mpango huo umeandaliwa kwa wakati muafaka kutokana na maandalizi ya mashindano makubwa ya riadha yanayotarajiwa kuanza mwezi Agosti mwaka huu, huku ukilenga kuwaunganisha mashabiki wake waliopo ndani na nje ya nchi katika safari ya kuendeleza mchezo huo.
Alisema kupitia kampeni hiyo, mashabiki watapata nafasi ya kushiriki moja kwa moja katika safari yake ya mafanikio kwa kukimbia naye au kuchangia fedha zitakazotumika kusaidia maendeleo ya vijana wenye vipaji vya riadha.
“Tunataka watu wawe sehemu ya ushindi huu ,Kila hatua ninayopiga iwe fursa kwa Watanzania kushiriki katika kusaidia kuibua na kuendeleza vipaji vya vijana ambao baadaye wataiwakilisha Tanzania katika mashindano mbalimbali ya kimataifa,” alisema Simbu.
kwa upande wake meneja wa Simbu Mosses Simon alifafanua kuwa awamu ya kwanza ya programu hiyo itafanyika katika mikoa ya Arusha, Dar es Salaam na Mwanza, ambako atakutana na mashabiki wake na kushiriki nao shughuli mbalimbali za michezo pamoja na mazoezi ya pamoja.
Alibainisha kuwa lengo kuu la Simbu Foundation ni kuandaa kizazi kipya cha wanariadha watakaokuja kufuata nyayo zake na za wanariadha wengine walioiweka Tanzania kwenye ramani ya dunia kupitia riadha.
“Tunachokifanya ni kuhakikisha tunawasaidia vijana wenye vipaji kupata fursa za mafunzo na maendeleo, tunahitaji kuandaa kina Simbu wengine watakaoiwakilisha Tanzania na kuendelea kupeperusha bendera ya taifa katika mashindano ya kimataifa,” alisema.
Aliongeza kuwa fedha zitakazopatikana kupitia kampeni hiyo zitatumika kuwasaidia vijana kupata mafunzo, vifaa vya michezo na fursa za kushiriki mashindano mbalimbali yatakayowawezesha kufikia viwango vya juu vya ushindani.
j
Kwa upande wake, Kaimu Katibu Mkuu wa Shirikisho la Riadha Tanzania (RT), John Lugane Manyama Junior, alisema shirikisho hilo linaunga mkono kwa asilimia mia moja juhudi zinazofanywa na Simbu Foundation kwa kuwa zinaendana na malengo ya kuendeleza riadha nchini.
Manyama alisema shirikisho limekuwa likitembea bega kwa bega na Simbu tangu mwanzo wa safari yake ya riadha na linafurahishwa kuona mwanariadha huyo akirejesha mchango wake kwa jamii kupitia programu za kuibua na kukuza vipaji vya vijana.
“Shirikisho la Riadha Tanzania ni mlezi wa wanariadha wote nchini ,hivyo, tunatoa baraka zetu kwa programu hii kwa sababu inalenga kuandaa wanariadha wa baadaye ambao watakuja kuliwakilisha taifa katika mashindano mbalimbali,” alisema.
Alieleza kuwa maendeleo ya riadha yanahitaji uwekezaji wa muda mrefu unaoanzia ngazi za chini kabisa, huku akisisitiza kuwa mchakato wa kuandaa wanariadha wa baadaye huanza kwa kutambua na kulea vipaji katika jamii.
“Tunapozungumzia maandalizi ya kizazi kijacho cha wanariadha, lazima tuanze kwenye ngazi za msingi, hapa ndipo tunapopata vijana watakaokuja kuchukua nafasi za wanariadha waliopo sasa na kuendeleza mafanikio ya Tanzania,” alisema.
Manyama aliongeza kuwa ushirikiano kati ya Shirikisho la Riadha Tanzania na Simbu Foundation utasaidia kuongeza idadi ya vijana wanaojitokeza kushiriki mchezo wa riadha, hatua itakayoongeza ushindani na kuimarisha uwezo wa taifa katika mashindano ya kikanda na kimataifa.
Alisema mafanikio ya wanariadha kama Simbu yanapaswa kutumika kama darasa na chachu kwa vijana wengi zaidi kujiunga na mchezo wa riadha, huku wadau mbalimbali wakihimizwa kuendelea kuwekeza katika maendeleo ya michezo ili kujenga taifa lenye wanariadha bora wa siku zijazo.
Kupitia kampeni hiyo, Simbu Foundation inatarajia kuwafikia mamia ya vijana katika maeneo mbalimbali nchini, ikiwa ni sehemu ya mkakati wa muda mrefu wa kuimarisha riadha na kuhakikisha Tanzania inaendelea kuzalisha wanariadha wenye uwezo wa kushindana katika viwango vya juu duniani.







0 Comments:
Post a Comment
unashauriwa kutoa maoni muda na wakati wowote na kama unahabari yeyote unaruhusiwa kututumia