WAZIRI SHEMDOE AAGIZA UJENZI WA BARABARA ZA AFCON KUJENGWA USIKU NA MCHANA*

 



- *_Amshukuru Rais Samia kwa kutoa fedha kwa wakati, ujenzi wa uwanja na barabara za AFCON_* 





Aagiza uadilifu katika usimamizi na utoaji wa fidia kwa waliopisha ujenzi wa barabara_* 


_Rc Makalla aeleza kuanza kwa ujenzi wa barabara za kuunganisha uwanja wa ndege KIA na uwanja wa AFCON_


Aaahidi kusimamia maelekezo yote ya serikali ili miradi hiyo ikamilike kwa wakati


Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (OWM -TAMISEMI) Prof. Riziki Shemdoe amemshukuru Rais wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa uwekezaji mkubwa alioufanya Mkoani Arusha katika ujenzi wa barabara kuelekea katika mashindano ya Mpira wa miguu kwa Mataifa ya Afrika (AFCON 2027) inayotarajiwa kuchezwa katika Mikoa ya Arusha, Dar Es Salaam na Visiwani Zanzibar.


Profesa Shemdoe ametoa shukrani hizo leo Jumapili Juni 14, 2026 wakati wa ziara yake Mkoani Arusha, akiambatana na Mkuu wa Mkoa wa Arusha Mhe. CPA Amos Gabriel Makalla na viongozi wengine wa Serikali na Chama Cha Mapinduzi CCM, kukagua mradi wa uwanja wa AFCON pamoja na barabara ya kuingia katika uwanja huo unaojengwa kwenye Kata ya Olmot, Jijini Arusha, akiagiza kasi zaidi katika kukamilisha kazi hizo.


"Kwa kazi hizi kwakweli najisikia fahari kuwa Mtanzania. Nielekeze kazi ya ujenzi wa barabara ifanyike usiku na mchana, niagize pia uadilifu katika usimamizi na utoaji wa  fidia kwa wananchi waliopisha ujenzi wa barabara hii. Nimshukuru sana Mhe. Rais kwa kutoa zaidi ya Shilingi Bilioni 80 ya ujenzi wa barabara hizi na zipo pia Bilioni 14.8 kwaajili ya fidia kwa wananchi." Amesema Mhe. Waziri.


Kwa upande wake Mhe. Makalla ameahidi kusimamia kikamilifu maelekezo yote ya Mhe. Waziri Shemdoe, ikiwemo usimamizi wa ujenzi wa uwanja huo wa AFCON pamoja na miundombinu ya barabara na maboresho ya viwanja vya ndege, ikiwemo barabara za kutoka Uwanja wa Ndege wa Kilimanjaro mpaka kufika katika uwanja huo wa Michezo.


Mapema katika maelezo yao, Msimamizi wa uwanja wa AFCON kutoka Wizara ya Habari, Utamaduni, sanaa na Michezo Bw. Martin Chomo na Mkurugenzi wa barabara kutoka Wakala wa barabara za Vijijini na Mijini TARURA, Injinia Venant Komba, wameeleza kuhusu maendeleo ya miradi hiyo na kuahidi kukamilisha kwa wakati ikiwemo viwanja vidogo vitano vitakavyotumika kwaajili ya mazoezi kwa Timu zitakazopangiwa kucheza Michezo yake Mkoani hapa.





About Woinde Shizza

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 Comments:

Post a Comment

unashauriwa kutoa maoni muda na wakati wowote na kama unahabari yeyote unaruhusiwa kututumia