Ticker

6/recent/ticker-posts

OLJORO NAMBA 5 WAISHUKURU RUWASA

 


WAKAZI wa Vijiji vya Losinyai na Einot Kata ya Oljoro Namba tano Wilayani Simanjiro Mkoani Manyara, wameishukuru Mamlaka ya maji safi na usafi wa mazingira vijijini (RUWASA) kwa kuwafikishia mabomba ya maji ili kukamilisha mradi wao aaaa maji kutoka mkoani Arusha.


Diwani wa kata ya Oljoro Namba 5, Loishiye Lesakwi, amesema wananchi wa eneo hilo wanashukuru kwa kupokea mabomba hayo ili kuendeleza mradi huo wa maji.


Lesakwi amesema mradi huo wenye thamani ya shilingi milioni 383 pindi ukikamilika utaweza kunufaisha wakazi wa vijiji vya Losinyai na Einot pamoja na mifugo ya eneo hilo.


Amesema mtandao wa mabomba ukishafungwa kwenye mradi huo ambao umefikia asilimia 67 wanatarajia utakamilika hivi karibuni na jamii kuanza kutumia maji.


Amesema wanaishukuru Serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Rais Samia Suluhu Hassan kwa kuwapambania wananchi wa Oljoro Namba 5 kwa kutoa fedha za kufanikisha mradi huo.


"Tunawashukuru RUWASA Mkoa wa Manyara na RUWASA Wilaya ya Simanjiro kwa kuendelea kufanya kazi kubwa na nzuri na tunatarajia mabomba yatafika site na kuanza kufungwa ili kukamilisha mradi," amesema Lesakwi.


Amesema anatarajia mara baada ya mtandao wa mabomba kuanza kusambazwa kwenye maeneo yaliyobaki, jamii na mifugo watapata fursa ya kunufaika na maji hayo.


"Mabomba yamefika hivyo tunawaomba yaende kufungwa kwani kazi kubwa mno RUWASA wamefanya hivyo tunasubiria matokeo mazuri kupitia mradi huu," amesema Lesakwi


Amesema RUWASA kupitia kauli mbiu yao ya Maji Bombani, wanatarajia wananchi wa Oljoro Namba tano watanufaika na mradi huo hivi karibuni pindi ukikamilika kwa maji kufikishiwa bombani kisha nyumbani.


Mkazi wa kijiji cha Losinyai, Sinyati Lazaro ameishukuru RUWASA kwa kufikisha mabomba hayo ya maji hivyo wanatarajia ndoto yao ya muda mrefu ya kupata maji itatimia.


"RUWASA na maji bombani tunatarajia itatufikia hivi karibuni mara baada ya mabomba kufika kijijini kwetu kwani mradi umeshafikia zaidi ya nusu ili kukamilika kwake," amesema Sinyati.

Post a Comment

0 Comments