Ticker

6/recent/ticker-posts

BALOZI KARUME AWASAA DADA ZAKE ZANZIBAR

Na Mwandishi Wetu, Zanzibar 

Balozi Mstaafu Ali Abeid Karume amesema uamuzi wa mdogo wake wa kike kuhama CCM  na kujiunga CUF hakuutegemea hivyo amemsihi ni vyema akautumia ubini wa jina la mumewe kuliko kuendelea kulitumia jina la hayati Sheikh Abeid Amani Karume akiwa upinzani. 

Amesema Mzee Katume katika maisha yake alipingana na wapinzani na usuktan uliowakandamiza waafrika katika visiwa vya Unguja na Pemba hadi yalipofanyika Mapinduzi mwaka 1964 hivyo mwanawe yeyote kwenda upinzani ni mambo ya kushangaza. 

Balozi Karume ameeleza hayo jana mjini unguja katika mahojiano maalum kufuatia uamuzi wa mdogo wake wa kike aitwaye Aksa Abeid Karume kuhama CCM na kujiunga na CUF . 

Alisema anaelewa fika kwamba mdogo  wake bila shaka atakuwa amezidiwa  nguvu za ushawishi toka kwa mumewe amaye amewahi kuwa mgombea mwenza wa urais wa jamhuri ya muungano wa Tanzania kupitia cuf Nassor Khamis Mohamed.

"Sikutegenea kumsikia mdogo wangu Aksa akipitisha uamuzi huu, pamoja na kuwa ana uhuru wa kuchagua lolote, amechagua jambo ambalo halina asili wala mnasaba na familia ya baba yetu" Alisema Balozi Karume. 

Aidha Balozi huyo mstaafu ambaye ni Waziri wa Mawasiliano na Uchukuzi wa SMZ, alisema mara nyingi wanawake wanapoolewa hutumia majina ya waume zao hivyo itakuwa  busara kwa Aksa akatumia jina mumewe na kuacha la m
Mzee Karume.

Alipotakiwa kueleza uamuzi huo umeiathiri kwa kiasi gani familia yao, Balozi huyo alisema heshima ya Mzee Karume itaendele kubaki mahali pale pale na wala haitavunjika kwa sababu tu miongoni mwa mwanawe  atahama ccm na kwenda upinzani. 

"Heshima ya Mzee wetu haitavunjika kwa mtoto au mjukuu wake yeyote kujiondoa CCM  na kwenda upinzani, Mzee aliyatoa  muhanga maisha yake kuwatetea wananchi wanyonge hadi wakapata uhuru na ukombozi kamili, tunaojua na kufahamu kamwe hatutayumba "Alieleza Balozi huyo .

Balozi huyo alikosoa hatua ya kaka yake ambaye alikuwa Rais Dk Amani Karume kumpa uwaziri Mansoor Yussuf Himid huku akijua babu yake marehemu Mohamed Sakum jina ndiye aliyekuwa katibu Mkuu wa ZNP kilichokuwa kikishindana kisera na ASP kuelekea uhuru wa Zanzibar dhidi ya ukoloni. 

"Sikuzishangaa kedi na ukorofi wake dhidi ya sera na misimamo ya ccm  ukifanywa na Mansoor hadi akafukuzwa CCM,  mapema nilishtuka kusikia amepewa uwaziri  na shemeji yake, kujiunga kwake CUF na kuipinga CCM  ni jambo lililotegenewa "Alisisitiza Balozi Karume. 

Hata hivyo Balozi huyo mstaaafu ambaye ni mjumbe wa halmashauri kuu ya CCM alisema CCM  ni taasisi kamili ya kisiasa hivyo haiwezi kudhoofika au kufa kwasababu tu mtoto mmoja au wawili wa mwanamapinduzi yeyote au Jemedari wa Mapinduzi kujiondoa  na kujiunga upinzani .

Pia alieleza kuwa yeye na watoto wake wataendelea kubaki CCM huku wakijua huwezi kuitaja CCM  bila kuvitaja TANU na ASP na ASP ndicho chama kilichoongozwa na hayati Mzee Abeid Karume hatimaye akawa Rais wa Kwanza  Zanzibar na Makamo wa kwanza wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania .

"Mzee wetu kwa kushirikiana na Mwalimu Julius Nyerere ndiyo waliounda Taifa la Tanzania.Taifa hili haikuachwa na wakoloni, Ni  jipya  lililoundwa kutokana na kuthamini umoja na uzalendo, maarifa na kutazama maslahi mapana ya kijamii "Alieleza Balozi Karume ambaye ni mtoto wa pili wa hayati Mzee Abeid Karume .

"Namshamgaa Aksa mbona wakati kaka yake Amani Karume akiwa Rais hakutangaza kuhama CCM ,kwanini afanye hivyo sasa, madai ya kusema anaunga mkono harakati za ukombozi , ukombozi na uhuru kamili wa zanzibar uliletwa na baba yake kupitia ASP 'Alisema. 

Post a Comment

0 Comments