Ticker

6/recent/ticker-posts

TADE:YATAKA BUNGE LIHESHIMIWE NA WABUNGE HAO


Image result for PICHA YA BUNGE
Na Umar Mukhtar , Zanzibar 

Chama cha ADA Tadea kimewataka Wabunge na Wajumbe wa Baraza la Wawakilishi kuvihamu  vyombo hivyo vinaendeshwa kwa taratibu zake maalum kwa kufuata kanuni zilizotungwa kisheria  hivyo Mbunge au Mwakilishi atakayekiuka taratibu zilizopo lazima ataadhibiwa kwa mujibu wa kanuni. 

Pia Chama hicho kimesema kila mhimili wa dola una taratibu na kanuni zake kwani bila uwepo wa  kanuni za uendeshaji,  vyombo hivyo vingekabiliwa na mabishano, misuguano pia mivutano isio ya suluhisho wala ukomo. 

Hayo yameelezwa jana mjini unguja   na Mkurugenzi wa Habari, Uenezi na Mawasiliano kwa Umma wa ADA Tadea, Rashid Yussuf Mchenga kufuatia uamuzi wa Spika wa Bunge Job Ndugai kuwasimamisha wabunge wawili wa Chadema, Halima Mdee na Ester Bulaya.

Mchenga alieleza kuwa Mabunge na Mabaraza yote ya Wawakilishi duniani huongozwa na kanuni zilizotungwa na kujipangia baada ya kupitishwa katika taratibu halali na kwamba Mbunge au Mwakilishi atakayekiuka huadhibiwa bila kutazamwa usoni . 

"Ingelikuwa Mahakama ni bustani basi maji yake ni ushahidi kwa mujibu wa sheria, tufahamu kuwa utawala huongozwa kwa kufuata sheria na katiba huku  mabunge yote duniani  yako chini ya kanuni zake zilizotungwa na kukubaliwa "Alisema Mchenga. 

Aidha alisema ni makosa kusema Mbunge au Mwakilishi fulani amefukuzwa kwa utashi wa Spika kwasababu Spika hutoa maamuzi kwa mujibu wa kanuni zilivyo na kwenye kamati ya Nidhamu na Maadili kiongozi wa upinzani huwa ni mjumbe mshiriki. 

"Spika ni kiti si mtu, hana maamuzi wala uwezo wa kutenda na kuamua jambo ikiwa suala hilo halina nguvu za kikanuni, Mbunge au Mwakilishi anapotimuliwa na kupewa adhabu ni wazi atakuwa amevunja na kukiuka kanuni halali "Alisisitiza. 

Kiongozi huyo wa upinzani aliwataka Wabunge na Wawakilishi kujiheshimu kwasababu hadhi na daraja zao mbele ya jamii hazilingani na makuli wa bandarini,wateja wa unga au wapiga debe kwenye vituo vya mabasi ya daladala. 

Mchenga alisisitiza kuwa kila mhimili una taratibu zake, mfumo wake na kanuni husika hivyo kutofuata na kutii taratibu hizo ni kuiitafutia matatizo ya kujitakia na yamapomkuta madhila mbunge au Mwakilishi hastahili kupewa pole au kusikitikiwa. 

"Haiwezekani vyombo vya Bunge au Baraza la Wawakilishi vikaendeshwa kama kundi la walevi  wako katika vilabu vya pombe, vyombo hivyo vina staha na miiko yake, jamii inawakilishwa na vyombo hivyo na katu  si busara uhuni na ukorofi kuwa sehemu ya bunge au baraza "Alisisitiza . 

Akitoa mfano alisema Bunge maalum  la katiba lilipoundwa na kukosekana mfumo wa kanuni lilikuwa kama soko kuu la kariakoo au la darajani zanzibar kwa kuhanikiza  kelele, mipasuko na malumbano lakini kanuni pale zilipotungwa kila mmoja aliheshimu na kutii taratibu. 

"Tulizoea kuwaona wabunge wa nchi moja jirani wakirushiana viti na kupigana ngumi mara kadhaa, tokea waboreshe kanuni zao sasa wamekuwa waungwana, wastaarabu na wenye kutambua hadhi na heshima yao ndani ya bunge "Alieleza Mchenga .

Hata hivyo Mkurugenzi huyo wa ADA Tadea aliiwahimiza na kuwashauri wabunge na wajumbe wa Baraza la  Wawakiiishi kufuata na kuheshimu kanuni zilizotingwa na kwamba vituko, mikasa na mizozo wanayoianzisha kimsingi haitoi taswira njema katika jamii kulingana na daraja zao.

Post a Comment

0 Comments