Ticker

6/recent/ticker-posts

GUNIA 168 ZA BANGI ZAKAMATWA MKOANI ARUSHA


WATU 20 wamekamatwa kwa kukutwa na shehena ya bangi gunia 168 katika kitongoji cha Engendeko, Kijiji cha Losinoni wilayani Arumeru mkoani hapa.
Akithibitisha kukamatwa kwa shehena hiyo ya bangi alfajiri ya kuamkia jana, Kamishna wa Intelijensia wa Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya nchini, Fredrick Kibute alisema ofisi yake ilishirikiana na askari wa Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) kutoka Oljoro ili kufanikisha kazi hiyo.

“Tulipata taarifa kutoka kwa raia wema na wiki iliyopita tukatuma kikosi maalumu kwa ajili ya uchunguzi na baada ya kupata taarifa za uwepo wa bangi hiyo tulipanga safu ya kikosi kazi kwa ajili ya kuja Arusha kukamata bangi hiyo ambayo awali wananchi hao waligomea uongozi wa wilaya baada ya kutakiwa kukisalimisha,” alisema Kibute.

Kwa mujibu wa Kibute, aliondoka saa nane usiku jana kuelekea katika kijiji hicho akiwa na kikosi maalumu kutoka ofisini kwake, wanajeshi pamoja na polisi na majira ya saa 10.00 alfajiri waliwasili katika kitongoji hicho na kuanza msako wa nyumba kwa nyumba.

“Kijiji cha Losinoni hasa kitongoji cha Engendeko ni eneo la kipekee ambalo limetia fora katika kilimo cha bangi na kuificha bila kukamatwa, lakini tulitumia intelijensia ya hali ya juu kuhakikisha tuwakamata wote pamoja na bangi walizokuwa nazo ndani ya nyumba zao za kuishi,” alifafanua.

Kamishina Kibute alitumia fursa hiyo kuwaonya wananchi wa Wilaya ya Arumeru kuacha mara moja tabia hiyo ya kulima bangi na kuwataka wasome alama za nyakati badala ya kufanya kilimo hicho kwa mazoea.

“Wanaojihusisha na kilimo cha bangi waache wasome alama za nyakati, ukiwa bondia usiogope ngumi za usoni ngumi zetu ni Sheria Namba Tano ya Mwaka 2010 ambayo sasa inasimamiwa kikamilifu ili kuhakikisha tunadhibiti dawa za kulevya hapa nchini kwani imeharibu maisha ya vijana wengi ambao ni nguvu kazi ya taifa,” aliongeza.

Kwa upande wake, Luteni Moses Gimonge kutoka Kikosi cha 833 Oljoro, alisema kazi hiyo haikuwa rahisi kutokana na kijiji hicho kuwa na milima na mabonde makubwa ambapo wananchi walitoka ndani ya nyumba zao na kukimbia, lakini waliwakabili kikamilifu na kuhakikisha wanatia mbaroni bila ya hata mmoja kukimbia.

Serikali ya Wilaya ya Arumeru tangu Agosti mwaka jana ilianza kupambana na kudhibiti kilimo cha bangi katika kata 14 na vijiji 22 ambavyo vilikuwa vinategemea kilimo cha bangi kama kitega uchumi cha kujipatia kipato. Alisema baadhi ya vijiji vimeachana na biashara hiyo haramu na kuanza kulima mazao aina ya mahindi, alizeti na pareto

Post a Comment

0 Comments