Na Woinde Shizza
Ujenzi wa kituo kidogo cha Polisi cha Morombo kilichopo kata
ya Murieti halmashauri ya Jiji la Arusha huenda ukawa mkombozi mkubwa kwa wakazi wa
eneo hilo ambalo linakuwa kwa kasi kibiashara na ongezeko la idadi ya watu.
Uwepo wa kituo hicho
utawezesha kusogeza huduma ya kiusalama kwa wakazi hao kwa ukaribu zaidi lakini
pia kesi zao zitaripotiwa hapo hapo badala ya Kituo kidogo cha Sombetini au
kituo Kikuu ambavyo vipo umbali mrefu toka eneo hilo.
Akizungumza katika eneo la kituo hicho, Kamanda wa Polisi
mkoa wa Arusha Naibu Kamishna (DCP) Charles Mkumbo alisema kwamba ufunguzi wa
kituo hicho ambacho kipo kwenye hatua za umaliziaji unatarajia kwenda sambamba
na wa nyumba za askari watakaofanya kazi kituoni hapo na hiyo itasaidia askari
kutoa huduma kwa haraka na ukaribu kwa kuwa watakuwa wanaishi eneo hilo.
Kamanda Mkumbo alisema kwamba, yeye pamoja na askari wapatao
200 wa vikosi mbalimbali jana waliamua kushiriki katika kuchimba msingi na
kubeba udongo “Vifusi” kutoka eneo la ujenzi na kwenda kuumwaga kwenye mtaro.
Alisema pamoja na majukumu walionayo ya kuhakikisha jiji la
Arusha pamoja na wilaya nyingine za mkoa huu zinakuwa salama lakini pia wameamua
kufanya hivyo kwa nia ya kupunguza gharama na watakuwa tayari kushiriki katika
kusogeza matofali kwa mafundi na hata kukoroga zege pindi nguvu kazi itakapohitajika.
“Pamoja na sisi kujitoa kufanya kazi hizi lakini pia wananchi
wanaozunguka eneo hilo wanapaswa kujitolea kubeba vifusi kwa kuwa kituo hicho
ni cha kwao”. Alitoa wito huo Kamanda Mkumbo.
Kwa upande wake mkazi wa eneo hilo aliyejulikana kwa jina la mzee
Isihaka Kivuyo alisema kwamba, kituo hicho kitasaidia kuiweka jamii karibu na jeshi hilo
jambo ambalo litasaidia kupunguza uhalifu.
Alisema kwamba wananchi wanatakiwa wafurahie ujenzi wa kituo
hicho hivyo na kuwataka wajitolee katika shughuli ndogondogo za ujenzi wa
nyumba hizo za askari badala ya kazi hizo kufanywa na askari Polisi pekee ambao
wana majukumu mengine ikiwemo kuhakikisha usalama wa wananchi na mali zao
unakuwepo.
Ujenzi wa kituo hicho chenye hadhi ya daraja B ambao
umefadhiliwa na Kampuni ya Lodhia Group ulianza toka mwaka 2016 mwezi Mei,
lakini pia ujenzi wa nyumba saba za askari kwa sasa upo kwenye hatua za uchimbaji
wa msingi na unatarajiwa kwenda kwa kasi ili uende sambamba na ufunguzi wa
kituo.
0 Comments
unashauriwa kutoa maoni muda na wakati wowote na kama unahabari yeyote unaruhusiwa kututumia