Waziri wa Mambo ya
Ndani Mh. Mwigulu Nchemba leo Mchana ametembelea jijini Arusha na kujionea
maendeleo ya ujenzi wa nyumba za Polisi zinazoendelea kujengwa baada ya ajali
ya moto iliyotokea mwishoni mwa mwezi Septemba ambayo ilisababisha familia za askari
13 kuunguliwa vitu mbalimbali na kukosa makazi.
Mh. Mwigulu alitumia
fursa hiyo kwa kuishukuru kamati ya Ulinzi na Usalama ya mkoa ambayo
inaoongozwa na Mkuu wa mkoa Mh. Mrisho Gambo lakini pia aliwashukuru wadau
ambao wote kwa pamoja walichukua hatua za haraka za kurejesha makazi ya askari
ambao walikumbwa na janga la moto huku akisisitiza kwa kusema kwamba hali
ilioonyeshwa na wadau hao ni mfano mzuri wa kuigwa na mikoa mingine waone nchi
inajengwa na wananchi.
Alisema kwamba suala
la makazi ya askari lipo katika kipaumbele cha serikali na Mh. Rais wa Jamhuri
ya Muungano wa Tanzania ameonyesha kwa vitendo katika maeneo tofauti ikiwemo
hapa Arusha.
Alisema Serikali
ikishamaliza hilo itaendelea na utaratibu mwingine wa kujenga majengo ya kisasa
ili askari wapate makazi bora huku akimuagiza Kamanda wa Polisi mkoa wa Arusha
awafikishie salamu askari wa Arusha kwamba, Mh. Rais yupo pamoja nao na Wizara ipo
pamoja nao.
Naye Kamanda wa
Polisi Mkoa wa Arusha Naibu Kamishna (DCP) Charles Mkumbo mbali na kuendelea
kuwashukuru wadau hao kwa kujitolea na kumuunga mkono Mh. Rais ambaye alionyesha njia siku hiyo hiyo
usiku kabla hakujapambazuka kwa kutoa mchango wake kama Serikali, lakini pia alisema
bado milango ipo wazi kwa watu wengine ambao hawakuwa na taarifa juu ya tukio
hilo ili kulisaidia Jeshi la Polisi mkoa wa Arusha liweze kufanikisha ujenzi wa
makazi ya askari hao.
Kamanda Mkumbo
aliongeza kwa kusema ujenzi wa makazi bora ya askari mkoani hapa utasaidia
kuwaongezea morali zaidi wa kazi askari hao hali ambayo itazidi kuimarisha
usalama na shughuli za maendeleo kusonga mbele.
Jumla ya nyumba 29 za
askari katika moja ya kambi iliyoathirika na ajali ya moto zilianzwa kujengwa
toka tarehe 2 mwezi huu jijini hapa na saba ambazo zipo katika ngazi ya msingi
zinatarajiwa kujengwa katika kituo kidogo cha Polisi Morombo kata ya Murieti.
Picha
no. Waziri wa Mambo ya Ndani Mh. Mwigulu Nchemba akikaribishwa
akipokelewa na Kamanda wa Polisi mkoa wa Arusha Naibu Kamishna Charles
Mkumbo mara baada ya kuwasili kambi ya Polisi iliyopo jijini hapa ambapo
ujenzi wa nyumba za waathirika wa ajali ya moto unaendelea.
Picha
2. Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Arusha Naibu kamishna (DCP) Charles
Mkumbo akitoa maelezo mafupi kwa Waziri wa Mambo ya Ndani Mh. Mwigulu
Nchemba juu ya maendeleo ya ujenzi wa nyumba za askari Polisi
walioathirika na janga la moto.
0 Comments
unashauriwa kutoa maoni muda na wakati wowote na kama unahabari yeyote unaruhusiwa kututumia