Meneja Biashara wa Kampuni ya Tanga Cement Bw. Peet Brits akikabidhi mifuko ya Saruji Kamanda wa Polisi mkoa wa Arusha Naibu Kamishna (DCP) Charles Mkumbo |
Ujenzi wa nyumba za polisi jijini hapa unaendelea
Na Woinde Shizza, Arusha
Jeshi la Polisi mkoani hapa, limepokea jumla ya tani hamsini sawa na
mifuko elfu moja ya Saruji yenye thamani ya shilingi Milioni kumi na
Mbili na Laki Tano toka kampuni ya Saruji yaTanga (Tanga Cement) ili
ziweze kusaidia ujenzi wa nyumba za Askari wa Jeshi hilo ambalo hivi
karibuni walipatwa na majanga ya moto yaliyosababisha nyumba za familia
13 kuungua na kuteketeza karibu kila kitu.
Akipokea shehena hiyo kwa niaba ya Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini,
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Arusha Naibu Kamishna (DCP) Charles Mkumbo
aliishukuru Kampuni ya Tanga Cement kwa kujitoa na kutambua mchango wa
askari katika kuimarisha usalama, na kuahidi kusimamia ili ujenzi huo
kasi yake iongezeke.
Alisema mbali na Kampuni hiyo pia aliwaomba
watu wengine binafsi pamoja na Makapuni mengine waige mfano toka kwa
kampuni hiyo kuisaidia jamii hasa katika sekta mbalimbali kama vile
elimu, afya na majanga kama haya.
Kamanda Mkumbo pia alitumia
fursa hiyo kushukuru watu binafsi , makampuni, taasisi pamoja na
majeshi ya Ulinzi na Usalama kama vile Jeshi la Wananchi (JWTZ), Jeshi
la Polisi Kilimanjaro, Chuo cha Polisi Moshi na Jeshi la Magereza.
Wengine ni kiwanda cha Magodoro cha Tanfoam, kiwanda cha A to Z, Ofisi
ya Mwanasheria mkoani hapa, Green Valley School na Kampuni ya Otterlo
Business Corporation Ltd (OBC) pamoja na watu binafsi ambao walitoa
msaada wa fedha, Chakula, Saruji nguo pamoja na Magodoro.
Kwa
upande wake Meneja Biashara wa kampuni hiyo Bw. Peet Brits alisema
kwamba, wao kama kampuni wameweka mkazo kusaidia katika elimu, afya,
maendeleo ya Jamii pamoja na mazingira lakini kwenye majanga mbalimbali
kama vile ajali za moto.
Alisema kwamba anafahamu kazi
zinazofanywa na Jeshi la Polisi katika kudumisha usalama ambapo
unasaidia kuvutia mazingira mazuri ya kibiashara hapa nchini. Alisema
wametoa msaada huo ili usaidie kujenga makazi ya familia za askari.
Bw. Brits alisema anajua walichochangia hakiwezi kutosheleza lakini
wanaamini kitasaidia kwenye ujenzi wa nyumba hizo na kuzitaka kampuni
pamoja na taasisi kusaidia Jeshi la Polisi ambalo linaimarisha usalama
hali ambayo inasaidia kuweka mazingira mazuri ya kibiashara.
Familia 13 za Jeshi hilo mkoani hapa zilikosa makazi siku ya tarehe
27/09/2017 baada ya nyumba zao zilizopo katika moja ya Kambi za Polisi
kuungua kwa moto uliotokana na hitilafu ya umeme ulitokea muda wa saa
12:45 Jioni.
0 Comments
unashauriwa kutoa maoni muda na wakati wowote na kama unahabari yeyote unaruhusiwa kututumia