MAKONDA: KAMBI YA MATIBABU YAENDELEA KUGUSA MAISHA, ATOA WITO WA KUONGEZA NGUVU KATIKA HUDUMA ZA AFYA
Na Woinde Shizza, Arusha
Mbunge wa Arusha Mjini na Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Paul Christian Makonda, amesema kambi ya matibabu bila malipo inayoendelea jijini Arusha imeendelea kuwa faraja kwa maelfu ya wananchi, hususani familia zenye kipato cha chini ambazo zimeshindwa kumudu gharama za matibabu kwa muda mrefu.
Akizungumza katika siku ya tano ya kambi hiyo, Makonda alisema bado kuna mahitaji makubwa ya huduma za afya nchini, hivyo ni muhimu Serikali, taasisi mbalimbali na wadau wa afya kuendelea kushirikiana ili kuwafikia wananchi wengi zaidi.
Alisema wananchi wamejitokeza kwa wingi kupata huduma mbalimbali za uchunguzi, matibabu na ushauri wa afya, jambo linaloonyesha uhitaji mkubwa wa huduma hizo katika jamii.
Makonda alieleza kuwa kambi hiyo imewapa matumaini wananchi wengi waliokuwa wamekata tamaa kutokana na kushindwa kupata matibabu kwa wakati, huku akiwapongeza madaktari, wauguzi na wataalamu wa afya wanaoendelea kutoa huduma kwa kujitolea hususa ni mkurugenzi wa hospitali ya taifa ya muhimbili Dkt Dahlila Kimambo kwa kuongeza idadi ya madaktari bigwa mara .
Aidha, aliwataka viongozi katika ngazi mbalimbali kuendelea kuhamasisha wananchi kupima afya zao mapema ili kubaini na kutibu magonjwa kabla hayajafikia hatua kubwa.
Alisisitiza kuwa afya ni msingi wa maendeleo ya mtu mmoja mmoja na taifa kwa ujumla, hivyo juhudi za kuimarisha upatikanaji wa huduma bora za afya zinapaswa kupewa kipaumbele huku akiongeza kuwa
ofisi yake ya mbunge itahakikisha inatoa huduma hii ya matibabu bure kwa wananchi wake kila mwaka
Makonda pia aliishukuru Serikali ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan pamoja na wadau wote waliofanikisha kambi hiyo, akisema ushirikiano huo umeendelea kuokoa maisha na kurejesha matumaini kwa wananchi wengi wa Arusha na maeneo ya jirani.
Pia aliwahimiza wananchi kutumia kikamilifu fursa ya kambi hiyo kwa kufika kupima afya na kupata matibabu bila malipo kabla ya zoezi hilo kukamilika
0 Comments:
Post a Comment
unashauriwa kutoa maoni muda na wakati wowote na kama unahabari yeyote unaruhusiwa kututumia