Ticker

6/recent/ticker-posts

MULONGO ALILIA AMANI


Mkuu wa mkoa wa Arusha,Magesa Mulongo ametamka ya kwamba miongoni mwa mambo ambayo yamekuwa yakimnyima usingizi na hata kumuumiza kichwa  ni pamoja na suala la kukosekana kwa amani na usalama katika mkoa wa Arusha.

Mulongo,alitoa kauli hiyo mwishoni mwa wiki iliyopita katika mkutano wa kujadili suala la amani na usalama katika mkoa wa Arusha ambao uliandaliwa na ofisi ya msajili mkuu wa vyama vya siasa hapa nchini.

Akiongea kwa hisia Mulongo alisema kuwa kiongozi yoyote anayeongoza mkoa usiokuwa na amani na usalama hata yeye binafsi anakosa amani moyoni hata kama akijifariji kwa kujifungia ofisini kwake.

“Unapoongoza  mkoa usiokuwa na amani unakosa amani wewe mwenyewe hata kama ukijifungia ofisini peke yako na kujifariji”alisema Mulongo

Hatahivyo,Mulongo alienda mbali zaidi na kudai ya kuwa vitendo na mazingira ya kutoaminiana tangu uchaguzi wa mwaka 2010 ndio sababu kuu iliyochangia vurugu katika baadhi ya maeneo ukiwemo mkoa wa Arusha.

Alisema kuwa mara baada ya uchaguzi huo kumalizika kuna baadhi ya watu wakiwemo wanasiasa walijitokeza hadharani na kuikataa serikali iliyoapishwa madarakani hivyo na kudai dhambi ile ilichangia kutafuna amani ya nchi  hadi sasa.

Mkuu wa mkoa huyo alimshukuru msajili wa vyama vya siasa nchini,Jaji Francis Mutungi kwa kuumiza kichwa kutafuta suluhu ya amani katika mkoa wa Arusha huku akihaidi ofisi yake kuhakikisha wanakamilisha maandalizi ya mkutano wa amani unaotaraji kufanyika desemba 6 mwaka huu jijini hapa.

Mbunge wa jimbo la Arusha mjini,Gobless Lema sanjari na mbunge wa viti maalumu,Mary Chatanda wote kwa pamoja walisema kuwa suala la amani katika mkoa wa Arusha limekuwa likiwaumiza vichwa mara kwa mara huku wakihaidi ushirikiano wa dhati na dola katika kutafuta suluhu ya amani hiyo.

Kwa kauli moja walisema kuwa siasa za ubaguzi na chuki zilichangia kwa kiasi kikubwa kupoteza amani ya mkoa wa Arusha huku wakidai kuwa watakuwa kielelezo cha amani kwa wanachama wao katika mkoa wa Arusha.

Katika mkutano huo mojawapo ya maazimio yaliyoafikiwa ni pamoja na kufanyika kwa mkutano mkubwa wa amani unaotaraji kufanyika desemba 6 mwaka huu katika uwanja wa Sheikh Amri Abeid ambapo vyama vyote vya siasa,waumini wa dini na wasio na dini sanjari na wakazi wa mji wa Arusha watashiriki kwa lengo la kuombea amani katika mkoa wa Arusha.

Post a Comment

0 Comments