Ticker

6/recent/ticker-posts

SEREKALI YAOMBWA KUANZISHA BODI YA ZAO LA UFUTA

 


Serikali imeombwa kuanzisha bodi ya zao la ufuta kama ilivyoanzisha bodi ya mazao ya pamba, kahawa na katani, ili kuwawezesha kuwanyanyua kiuchumi wakulima wa zao la ufuta ambalo hivi sasa linalimwa kwa wingi hapa nchini.

Imeelezwa kwamba bodi hiyo ya zao la ufuta endapo itaanzishwa itawasaidia wakulima wake kunufaika kiuchumi, kwani watakuwa na soko la uhakika kuliko hivi sasa wanapotapeliwa na walanguzi wanaonunua zao hilo shambani mwao.

Ombi hilo lilitolewa na baadhi ya wakulima wa zao la ufuta wa Tarafa ya Mbugwe, Wilaya ya Babati, katika Mkoa wa Manyara, ambao walijengewa uwezo wa kulima zao hilo na shirika lisilo la kiserikali la Farm Africa.  

Mmoja kati ya wakulima hao Theresia Njaiko mkazi wa kijiji cha Mwada, alisema endapo Serikali ingeanzisha bodi ya zao la ufuta wakulima wengi nchini wangefaidika kwenye uuzaji kupitia zao hilo linalolimwa kwa wingi nchini.

Mkulima mwingine wa ufuta Khadija Juma mkazi wa kijiji cha Magugu, alisema japokuwa zao hilo halina bodi kama mazao mengine ila wanategemea shirika la Farm Africa kwa kuwapatia elimu ya kilimo hicho, mbegu, dawa na masoko.

Tabu Issa wa Magugu aliiomba Serikali kutupia jicho kwenye zao hilo, kwani hivi sasa wakulima wengi wamefaidika kupitia ufuta hivyo Serikari iwageukie na wao, japokuwa wanawezeshwa na shirika hilo lisilo la kiserikali la Farm Africa.

Kwa upande wake, mkulima wa kijiji cha Mwada Lucas Said alilishukuru shirika la Farm Africa kwa kuwawezesha mafunzo, kuwapatia mbegu na kuwatafutia soko la ufuta, hivyo kuwasaidia kuwanyanyua kiuchumi kupitia zao hilo.

Mkulima Juliana Agustino wa Mwada, alitoa wito kwa Serikali iwasaidie wakulima wa ngazi ya chini, kuwawezesha kushiriki maonyesho ya kilimo ya nane nane ili waonyeshe mazao yao na pia kujifunza kupitia wakulima wengine.

Post a Comment

0 Comments