Ticker

6/recent/ticker-posts

NAMANGA YAPATA KITUO CHA AFYA

 

Mkuu wa Mkoa wa Arusha Mrisho Gambo amesema wananchi wa kata ya Kimokouwa na Namanga kwa ujumla hawana haja yakupata matibabu tena kutoka nchi jirani ya Kenya.

Aliyasema hayo alipokagua ujenzi wa kituo cha afya cha Eworendeke katika kata ya Kimokouwa wilayani Longido.

Gambo amesema kwa mda mrefu sana wananchi wa Namanga kwa ujumla walikuwa wanapata hadha yakufuata huduma ya matibabu Longido mjini au nchi jirani ya Kenya na hivyo kufanya wagonjwa wengi kutembea umbali mrefu.

Amesema kituo hicho cha afya kimepata mgao wa shilingi milioni 700 kutoka serikalini na wananchi wanachangia nguvu kazi katika kukijenga na mpaka sasa kiasi cha milioni 400 ndio kimeshatumika na ujenzi unaendelea.

Gambo amesema mbali na serikali kutoa kiasi hicho cha fedha bado bajeti ya ununuzi wa madawa umeongezwa kutoka bilioni 31 hadi bilioni 269 kwa mwaka huu wa fedha, na hii itasaidia huduma ya madawa kupatikana kiurahisi katika kila kituo cha afya na hospitali zote nchini.

Kituo cha afya cha Eworendeke kinatarajia kukamilika Agosti 2018 na huduma zote zitapatikana zikiwemo huduma za  upasuaji na x-ray, hivyo itarahisisha matibabu kwa wananchi wote wa Namanga.

Mkuu wa Wilaya ya Longido Daniel Chongolo,amesema asilimia 27 ya wajawazito walikuwa wanajifungulia katika vituo vya afya kwa wilaya nzima na idadi imeongezeka kufikia asilimia 35.

Chongolo amesema ongezeko hili litasaidia kupunguza vifo vya mama na mtoto katika wilaya yake.

Mgaga mkuu wa Mkoa Dokta Vivian Wonanji,amesema serikali imeshatenga kiasi cha fedha cha milioni 200 kwa ajili ya manunuzi ya vifaa kwa vituo vyote vya afya na hospitali kwa mkoa mzima na anaendelea na zoezi la kuongeza watumishi katika sekta ya afya.

Amesema agizo la serikali ni kuhakikisha vituo vyote vya afya vinakuwa na huduma ya x-ray, hivyo katika kituo hicho wanajenga chumba maalumu kitakachotoa huduma hiyo kwa wananchi wote wa Namanga.

Akitoa shukurani zake za dhati kwa serikali bwana Hassan Hamis ambae ni mkazi wa Namanga amesema kweli kituo hicho cha afya kitasadia kuondokana na hadha waliyokuwa wanaipata kufuata matibabu kwa umbali mrefu, na pia itapunguza vifo vilivyokuwa vinatokana na umbali huo.

Gambo anaendelea na ziara yake katika wilaya ya Longido ambapo ametembelea kituo kingine cha afya cha  Engarenaibor kilichogharimu kiasi cha milioni 200, pia ameshiriki ujenzi wa kituo cha afya cha kata ya Ketumbeine.

Post a Comment

0 Comments