Ticker

6/recent/ticker-posts

MMILIKI WA LODGE MAARUFU HAPA ARUSHA AITWA MAHAKAMANI

KESI inayomkabili raia wa Ujerumani,Andreas Tauscher anayekabiliwa na mashtaka ya  kuishi nchini kinyume na sheria imeendelea kuunguruma katika mahakama ya hakimu mkazi Arusha ambapo juzi mahakama hiyo imekubali kuitwa mara moja shahidi nambari nne katika kesi hiyo ambaye ni mmiliki wa hoteli ya Hatari Lodge ,Jeorge Gabriel ili aweze kuhojiwa kuhusu kauli  aliyoitoa  kwa maandishi mahakamani hapo.
 
Hatua hiyo imefuatia mara baada ya ombi la upande wa mlalamikaji ambao ni idara ya uhamiaji mkoani Arusha uliowakilishwa na wakili,Ngwijo Godfrey kudai kuwa Gabriel hayupo na hapatikani hivyo hawaoni haja ya raia huyo kufika mahakamani hapo kuhojiwa kuhusu kauli yake.

Wakili huyo upande wa walalamikaji ameiambia mahakama kwamba wao wanataka kufunga ushahidi  na hawaoni  haja ya raia kufika mahakamani hapo kuhojiwa kuhusu kauli yake kwa kuwa hapatikani ombi lililopingwa vikali na wakili upande wa mshtakiwa,Wilfred Mirambo.

Wakili wa upande wa mshtakiwa,Mirambo alipinga ombi hilo na kudai rai huyo wa nchini  Ujerumani yupo jijini Arusha na mara kwa mara
anaonekana katika mitaa mbalimbali hivyo ni vyema akafika mahakamani hapo na ahojiwe kuhusu kauli yake aliyoitoa kwa maandishi.

Mahakama hiyo chini ya hakimu mkazi,Mwankuga Gantwa baada ya
kusikiliza hoja kutoka pande zote mbili  iliridhia hoja ya wakili
Mirambo na kutaka iandikwe notisi ya kuitwa  mahakamani raia huyo
novemba 27 mwaka huu ili aweze kuhojiwa kuhusu kauli yake aliyoitoa kwa maandishi.

Katika kesi hiyo  nambari 128 ya mwaka 2013  raia huyo wa nchini
Ujerumani, Tauscher  ambaye alikuwa mfanyakazi wa hoteli ya Hatari
Logde  anakabiliwa na kosa la kuishi nchini kinyume cha sheria kwa
kutokuwa na hati ya kusafiria.

Kosa hilo linatajwa kuwa kinyume na sheria za jamhuri ya muungano wa Tanzania kifungu cha 31 (1) (i)  na cha 2 cha sheria ya uhamiaji
nambari 54 ya mwaka 2002.

Mnamo Aprili 18 mwaka huu raia huyo alikamatwa katika barabara ya
Afrika Mashariki wilayani Arusha na maofisa wa uhamiaji kwa kosa la
kuishi kinyuma na sheria za hapa nchini na kesi hiyo itasikilizwa tena
novemba 27 mwaka huu.

Post a Comment

0 Comments