Ticker

6/recent/ticker-posts

HOLILI YOUTH ATHLETIC CLUB (HYAC) ILIANZA KWA JUHUDI ZA MTU BINAFSI KAMA HIVI


Viongozi wa HYAC L-R (Nelson Mrashani,Domician Genand na Timoth Kamili

Holili Youth Athletic Club ni moja ya vilabu vya riadha vilivyoanzishwa hapa nchini, club hii ipo Holili wilayani Rombo Mkoa wa Kilimanjaro.  

Club hii ilianzishwa na mdau mkubwa wa mchezo wa riadha ambaye ni mkurugenzi kwa sasa DOMICIAN RWEZAURA GENANDI mnamo 2010 na kusajiliwa rasmi 2011 kwa namba ya usajili NSC9833 na kuanza shughuli za kuendeleza mchezo wa riadha mwaka moja baadaye.
Clu hii ilianza na wachezaji 6 tu lengo lake likiwa kuibua na kuendeleza vipaji vya vijana katika mchezo wa riadha hapa nchini, hadi sasa club ina jumla ya wanariadha 15 wakiwemo wazoefu wachache na chipukizi ambao kwa pamoja wamekuwa wakifanya vizuri katika mashindano mbalimbali walioshiriki ndani na nje ya nchi.
Malengo makubwa ya club hii ni kukuza na kuendeleza mchezo wa riadha kwa kuwalea wanariadha chipukizi ili waje kufanya vizuri baadaye, kuwepo kwa wanariadha wazoevu katika club kumewapa hamasa wale wachanga kwani wamekuwa wakiwaiga katika mazoezi na hivyo kuinua viwango vyao.
Matunda na mafanikio: Holili Youth Athletic Club kwa muda mfupi tangu kuanzishwa kwake imeanza kuonyesha matumaini ya kufufua heshima ya Tanzania katika anga za kimataifa katika riadha ambapo mpaka sasa imeshazalisha wanariadha wenye viwango vya kimataifa.
Katika mashindano mbali mbali yaliyofanyika hapa nchini washindi wa mbio karibu zote wametoka Holili Youth Athletic Club kwa mfano:
(1)Rotary Club 21km yaliyofanyika Dar 2012 mshindi alikuwa Dickson Marwa wa HYAC (2)Filbert Bayi 10km yaliyofanyika Karatu 2012 nafasi ya kwanza na ya pili zilikwenda kwa Dickson Marwa na Patrick Nyangero wa HYAC  (3)New Years Mid-Night Marathon iliyofanyika Dar 2012 nafasi ya kwanza na ya pili Dickson Marwa na Patrick Nyangero wa HYAC (4)Ngorogngoro Marathon iliyofanyika Karatu 2013 nafasi ya kwanza alishinda Dickson Marwa wa HYAC (5)Sokoine Memorial Mini Marathon 10km nafasi ya kwanza ilikwenda kwa Dickson Marwa wa HYAC. 
Pia katika Safari marathon ya Arusha na Kilimanjaro Marathon vijana wa Holili walichukua nafasi muhimu za mbele, katika mashindano ya taifa yaliyofanyika Morogoro  vijana wa Holili walifanikiwa kupata medali tano ambazo ni Gold tatu na Bronze mbili. Mafanikio hayo siyo ya kubezwa.
Changamoto: 
1)Upatikanaji wa vijana wenye vipaji kutoka sehemmu mbalimbali nchini, hili linatokana na uchanga wa club kwa wakati huu na vile vile ukosefu wa ushirikiano wa karibu kutoka kwa viongozi wa vyama vya riadha mikoani. 
2)Gharama kubwa za uendeshaji wa kambi za mazoezi, hili nalo linasababishwa na ukosefu wa wadhamini wa mchezo wa riadha hasa wadhamini wetu wa ndani (wadau na makampuni ya kibiashara).
Matarajio: Matarajio ya club ni kupambana vilivyo hadi kieleweke na hatimaye kufanya vizuri katika mashindano mbali mbali ndani na nje ya nchi, kubwa zaidi ni kuwa na wachezaji wengi katika timu ya taifa itakayoshiriki mashindano ya Jumuia za Madola zitakazofanyika 2014 Scotland na mashindano ya Olimpiki zitakazofanyia Rio De Janeiro Brazil 2016.
Nukuu: Domician Genand (Mkurugenzi), Nelson Mrashani (Meneja), Timoth J. Kamili (Kocha)

Post a Comment

0 Comments