Ticker

6/recent/ticker-posts

TAMASHA LA KUMSHUKURU MUNGU SASA KUFANYIKA DESEMBA 25 DIAMOND JUBILEE

 Mkurugenzi wa Kampuni ya Msama Promotions, Alex Msama akifafanua jambo kwa umakini mbele ya Waandishi wa habari (hawapo pichani) jijini Dar es Salaam, mwishoni mwa wiki kuhusu maandalizi ya tamasha la kumshukuru Mungu kwa amani na utulivu wakati wa Uchaguzi Mkuu litakalofanyika Desemba 25.

Mkurugenzi wa Kampuni ya Msama Promotions, Alex Msama akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam, mwishoni mwa wiki kuhusu maandalizi ya tamasha la kumshukuru Mungu kwa amani na utulivu wakati wa Uchaguzi Mkuu litakalofanyika Desemba 25.

KAMPUNI ya Msama Promotions imeamua kuandaa Tamasha la muziki wa Injili litakalofanyika katika Ukumbi wa Diamond Jubilee, jijini Dar es Salaam kwa lengo la kumshukuru Mungu nchi kuvuka salama katika Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 25.

Akizungumza jijini Dar es Salaam, mwishoni mwa wiki, Mkurugenzi wa Msama Promotions, Alex Msama, alisema wameamua kuua ndege wawili kwa jiwe moja, kwani sasa litafanyika Desemba 25, likibeba Sikukuu ya Krismasi na shukrani hiyo ya kuvuka salama katika Uchaguzi Mkuu.


Alisema kutokana na tamasha hilo kubeba ajenda hizo mbili kwa pamoja, kamati yake imelipa uzito mkubwa kwa upande wa suala la  maandalizi ambapo wameanza kuzungumza na waimbaji nguli wa kitaifa na kimataifa.

Msama alisema baada ya tamasha hilo kufanyika Desemba 25 katika Ukumbi wa Diamond Jubilee, litahamia katika mikoa mbalimbali itakayoteuliwa na kamati yake kwa kuzingatia kigezo cha wingi wa maombi na uwezo wao kifedha.

“Naomba ifahamike, tamasha hili la kumshukuru Mungu kuiwezesha nchi kuvuka salama katika mtihani mgumu wa Uchaguzi Mkuu uliokuwa na ushindani mkubwa, litafanyika Desemba 25 katika Ukumbi wa Diamond Jubilee,” alisema Msama na kuongeza:

“Unaweza kuona ni tamasha ambalo safari hii litakuwa na uzito mkubwa, kwani litakuwa limebeba uzito wa Krismasi itakayoambatana na shukrani maalumu kwa Mungu kutokana na kuijalia nchi kuvuka salama katika Uchaguzi Mkuu,” alisisitiza Msama.

Kuhusu waimbaji, Msama alisema kamati yake itajitahidi kuwaleta wenye uzito na mvuto kulingana  na uzito wa tamasha hilo, akiamini litakuwa na mvuto wa tofauti na yaliyotangulia na kuwasihi wapenzi na mashabiki wa muziki wa Injili kukakaa mkao wa kupokea baraka za Mungu.

Msama kupitia Kampuni yake ya Msama Promotions, amechangia kwa kiasi kikubwa kukua kwa muziki wa Injili nchini kupitia ubunifu wake wa kuratibu matukio ya muziki huo kuanzia tamasha la Pasaka, Krismasi na uzinduzi wa kazi za waimbaji mbalimbali.

Juhudi hizo za Msama ndizo zimeufanya muziki wa Injili kupata umaarufu mkubwa ndani na nje ya Tanzania kiasi cha kuwa moja ya ajira kwa vijana wenye vipaji na karama ya kumtumikia Mungu kwa njia hiyo ya uimbaji.

Post a Comment

0 Comments