JIJI ARUSHA KITOVU CHA MAFUNZO YA HALMASHAURI ZINGINE


 
Halmashauri ya Jiji la Arusha imekuwa ikipokea wageni kutoka miji mbalimbali ndani na nje ya nchi kwa ajili ya kujifunza mambo ya kiutendaji na hiyo ni kutokana na sababu za kiufanisi katika utendaji wa shughuli za kila siku zinazoigusa hasa jamii.
Halmashuri ya Jiji la Arusha imepokea wageni (Mameya, Mkurugenzi, Madiwani na baadhi ya Watendaji) kutoka halmashauri ya jiji la Dar Es Salaam  ambapo lengo kuu la ziara yao lilikuwa ni kujifunza juu ya usimamizi na uendeshaji wa Jalala la kisasa, usimamizi wa shughuli za kitalii katika jiji la Arusha hasa maeneo yenye vivutio na usimamizi pamoja na uendeshaji wa shughuli za Maegesho.
“Nimefarijika na ujio wenu katika halmashauri yetu na naamini mnayo mengi ya kujifunza na pia hii ni fursa kubwa kwetu pia kwani sio tu ziara ya kimafunzo bali ni muunganiko ambao una faida kubwa katika siku za baadae” alisema Mkurugenzi wa jiji la Arusha Ndg. Athumani Kihamia alipokuwa akitoa neno la ukaribisho kwa wageni.
“Kufuatia ziara yenu pia halmashauri yetu itaweza kubadilishana uzoefu na nyie katika Nyanja mbalimbali za kiutendaji na pia halmashauri yetu kuweza kujitangaza vizuri katika miji mingine hapa nchini na hata nje ya nchi” aliongeza Kihamia.
Naye mstahiki Meya wa Jiji la Arusha Mhe. Kalist Lazaro ameipongeza halmashauri ya Jiji la Dar Es Salaam kwa kuchagua Jiji la Arusha kama sehemu yao ya kujiongezea ujuzi.
Pamoja na ziraya yao ya kimafunzo pia walipata fursa ya kutembelea bustani inayoishi ya Themi (Themi Living Garden) ambayo katika historia hapo mwanzo ilikuwa kichaka cha wahalifu ila baadae Halmashuri ya Jiji la Arusha iliamua kuhifadhi eneo hilo na kuwa mahala pa mapumziko. Kwa sasa linasimamiwa na kampuni ya watu wa Itali, Oikos baada ya kuingia nao mkataba wa maridhiano juu ya utunzaji wa mazingira.
Kadhalika walipata fursa ya kutembelea mradi wa Shanga Shangaa ambao unaendeshwa na watu wenye ulemavu mbalimbali waliowezeshwa kufanya shughuli za utengenezaji wa bidhaa mbalimbali zinazotokana na vyupa, shanga, magazeti na malighafi za zamani na kuzitengenezea bidhaa mpya kwa ajili ya matumizi mbalimbali ya kila siku. Mradi huo ni rafiki wa wazingira.
Aidha Halmashauri ya Jiji la Arusha pia imepokea  Wataalam kutoka Jiji la  Mwanza, Manispaa ya Ilemela na Morogoro kujifunza masuala ya usafi na mazingira sambamba na uendeshaji na usimamizi wa shughuli za dampo la kisasa lilipo kata ya Murriet Jijini hapa mapema leo hii.

About Woinde Shizza

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 Comments:

Post a Comment

unashauriwa kutoa maoni muda na wakati wowote na kama unahabari yeyote unaruhusiwa kututumia