Ticker

6/recent/ticker-posts

ENDIAMTU YAKUSANYA ZAIDI YA MILIONI 21 KWA AJILI YA MFUKO WA ELIMU

KATA ya Endiamtu iliyopo Mji mdogo wa Mirerani Wilayani Simanjiro Mkoani Manyara,imefanikiwa kukusanya kiasi cha sh21.658 milioni za mfuko wa elimu kwa mwaka jana ambazo zimetumika kuinua elimu katika kata hiyo.

Akizungumza juzi kwenye kikao cha maendeleo cha kata hiyo (WDC) Ofisa mtendaji wa kata hiyo,Edmund Tibiita  alisema fedha hizo zilichangwa na wananchi mbalimbali wa vitongoji vinne vinavyounda kata hiyo.

Tibiita alisema kitongoji cha Kazamoyo walichanga sh8.3 milioni,Zaire walichanga sh2.7 milioni,Kairo walichanga sh750,000,kitongoji cha Sekondari walichanga sh2 milioni na kitongoji cha Kilimahewa walikusanya sh2 milioni.

Alisema askari polisi wakiongozwa na mkuu wa kituo cha polisi Mirerani ASP Ally Mkalipa,walitoa sh310,000 Diwani wa kata ya Endiamtu,Lucas Zacharia alijitolea sh3 milioni na wamiliki wa magari ya DCM walijitolea sh360,000.

“Wengine waliotuchangia ni marafiki wa Diwani wetu Lucas waliojitolea sh2 milioni,wafanyabiashara wa maduka sh830,000 na vifaa vilivyobambuliwa vina thamani ya sh375,000.” alisema Tibiita.

Naye,Diwani wa kata ya Endiamtu Lucas Zacharia,aliwataka wazazi na walezi wa kata hiyo kutoa kipaumbele na kuzingatia kuwapatia watoto wao elimu kwani kwa dunia ya sasa bila kuwa na elimu Taifa litakuwa gizani.

“Elimu iwe ndiyo ajenda yetu ya kwanza kwa sisi kata ya Endiamtu hivyo tujitahidi kwa kadiri ya uwezo wetu katika kuhakikisha kuwa watoto wetu wanapata elimu bora na iliyo katika mazingira mazuri,” alisema Zacharia.

Pia,alisema hivi sasa wanatakiwa kuweka nguvu moja kwenye ujenzi wa madarasa ya shule mpya ya msingi Zaire na Endiamtu,kwani shule za msingi Mirerani na Jitegemee hazina maeneo ya kujengewa madarasa mapya.

Aliwataka wajumbe wa kamati ya maendeleo ya kata hiyo (WDC) wajitolee kwa moyo mmoja,katika kuhakikisha kuwa wanawatumikia ipasavyo wananchi waliowachagua kwani huu siyo wakati wa kufanya siasa.

Post a Comment

0 Comments