Ticker

6/recent/ticker-posts

BARABARA YA VIGWAZA-BUYUNI-MWAVI YAHARIBIKA VIBAYA/RIDHIWANI AAHIDI KUSIMAMIA KERO HIYO


MBUNGE wa jimbo la Chalinze Ridhiwani Kikwete,akiangalia barabara kutoka Vigwaza-Mwavi iliyoharibika vibaya eneo la Buyuni hali inayosababisha magari kushindwa kupita.

 Mkazi wa Mwavi ,Zainab Zuberi akivushwa  kwenye maji yaliyokata barabara eneo la Buyuni,kwa kubembwa shingoni .
Mbunge wa jimbo la Chalinze Ridhiwani Kikwete,akizungumzia kero ya kuharibika kwa baadhi ya  miundombinu ya barabara kutokana na mvua zinazoendelea kunyesha,ambapo mvua iliyonyesha april 7 na 8 imesababisha kuharibu barabara ya Vigwaza-Buyuni-Mwavi na ya Milo-Kitonga-Ruvu.

Baadhi ya wakazi wanaotumia barabara ya Vigwaza-Buyuni-Mwavi wakipita kwa shida kutoka na barabara hiyo kuharibika vibaya kutokana na mvua.(picha na Mwamvua Mwinyi)

Na Mwamvua Mwinyi,Chalinze
MVUA kubwa iliyoambata na upepo mkali,imekata mawasiliano ya miundombinu ya barabara eneo la Buyuni, na kusababisha wakazi kutoka kata ya Vigwaza na Mwavi jimbo la Chalinze,kupata shida.
Hali hiyo inasababisha wakazi hao,kuvushwa kwa kupata msaada wa kubebwa mgongoni na shingoni kwa gharama ya sh.3,000 na 2,000 na pikipiki kupitishwa kwa sh.5,000 huku magari yakishindwa kupita kabisa.
Baadhi ya wakazi hao,akiwemo Zaina Zuberi aliekuwa akienda Mwavi,alisema wapo katika hali ngumu .
“Mvua hapa bado haijanyesha,maji haya yanatokea maeneo ya Msoga huko na kufika huku daraja la  Mbiki,Buyuni na kukatiza katika hii barabara,sipati picha mvua ikipiga hapa kwa mwezi huu”
“Barabara ni mbovu kama mnavyojionea,haipitiki,watu tunapata shida kufuata mahitaji ya nyumbani ,tatizo ni mkandarasi ,barabara imejengwa bila kuwekwa makaravati,kila akielekezwa kujenga kutokana na hali halisi ya barabara haiwi hivyo,”
Nao baadhi ya vijana wanaosaidia kuwavusha watu na pikipiki,akiwemo Rashid Juma,alisema tangu mvua ziharibu eneo hilo april 7 wanavusha watu kwa maelewano kulingana na uwezo wa mtu.
“Tunapata fedha kulingana na kichwa cha mtu au pikipiki,kila mtu mmoja 3,000 au 2,000 na pikipiki 5,000 “alieleza.
Aidha kutokana na mvua hizo,zimeathiri pia barabara nyingine ya kutoka Milo-Kitonga hadi Vigwaza.
Mbunge wa jimbo la Chalinze ,Ridhiwani Kikwete ,alitembelea barabara hizo  na kujionea hali halisi.
Ridhiwani alisema ,hali iliyopo hairidhishi na kuwapa wakati mgumu wakazi wa maeneo hayo,na ameahidi kuisimamia kero hiyo kwa kuifikisha bungeni na halmashauri ya wilaya ya Chalinze ili lifanyiwe kazi.
Alieleza kuna kila sababu ya mkandarasi kufanya kazi kulingana na uhalisia wa eneo husika hali inayosababisha wananchi kupata tabu na barabara kuharibika kila wakati.
Katika hatua nyingine Ridhiwani ,aliunga mkono juhudi za ujenzi wa darasa lililobomoka kutokana na mvua iliyonyesha april 7 ambapo amechangia kiasi cha sh.100,000,mabati 50,mifuko ya saruji 50 na nondo 20.
Alibainisha kwamba shule hiyo imejengwa miaka 40 iliyopita hivyo miundombinu yake pia imechakaa.
Ridhiwani alisema kuna kila sababu ya kuangalia namna ya kukarabati shule hiyo kwani majengo yake yamejengwa miaka mingi.
Afisa mtendaji  wa Kidogozero,Lilian Mbwa,alisema kila kaya itachangia matofali mawili na kila mjumbe wa serikali ya kijiji ni tofali 10.
Hata hivyo alisema halmashauri ya kijiji itachangia jumla matofali 200 na wadau wa maendeleo  matofali 300.
Mwishoni mwa wiki iliyopita,kaya zaidi ya 20 zimekosa makazi ya kuishi na nyumba zaidi ya  90 ziliharibika ,kubomoka na nyingine kuezuliwa mapaa huko jimbo la Chalinze,kutokana na mvua iliyoambatana na upepo mkali.
Maeneo yaliyokumbwa na adha hiyo ni Chalinze Mzee,Bwawa la umwangiliaji la Msoga ambalo limetoboka ,Msoga na shule ya Sekondari ya Imperial.

Post a Comment

0 Comments