BREAKING NEWS

Thursday, August 4, 2022

WANAHABARI IRINGA WAJIKITA KUTANGAZA UTALII NCHINI.

  

Kamishina msaidizi wa Hifadhi  ya Taifa  (RUNAPA), Godwell Ole Meng’atak akiongea na waandishi wa habari wakati wa ziara ya Iringa Journalists Ruaha The Royal Tour namna gani ambavyo hifadhi hiyo ya taifa imejaliwa kuwa na vivutio vingi vya kitalii kwa ajili ya watalii ambao watafanikiwa kutembelea hifadhi hiyo
Baadhi ya waandishi wa habari wa mkoa wa Iringa wakiwa kwenye picha ya pamoja na mwenyekiti wa waandishi wa habari mkoa wa Iringa Frank Leonard wakati wa ziara ya 
Iringa Journalists Ruaha the Royal Tour
Afisa Uhifadhi katika hifadhi ya taifa ya Ruaha, Amina Rashidi akiongea na waandishi wa habari wakati wa ziara ya Iringa Journalists Ruaha the Royal Tour
Baadhi ya waandishi wa habari wa mkoa wa Iringa wakiwa kwenye picha ya pamoja katika makumbusho ya chifu Mkwawa yalipo kalenga wakati wa ziara ya Iringa Journalists Ruaha the Royal Tour

 


Na Fredy Mgunda,Iringa.

KAMISHINA msaidizi wa Hifadhi  ya Taifa  (RUNAPA), Godwell Ole Meng’ataki amesema kuimarishwa kwa ushirikiano baina ya Sekta ya Utalii na vyombo vya habari nchini kutachochea  ongezeko zaidi la watalii wa ndani na nje ya nchi hatua itakayosaidi kukuza pato la Taifa na uboreshwaji wa huduma kwa wananchi.

Akizungumza wakati wa ziara ya waandishi wa habari wa mkoani Iringa (Iringa Journalists Ruaha the Royal Tour) ambapo waandishi wapatao 40 waliotembelea hifadhi ya Taifa Ruaha,Kamishina Msaidizi Meng’ataki alisema kuwa mategemeo yake kuwa ziara ya namna hiyo italeta tija katika sekta ya utalii kwa kuufahamisha umma kuhusu umuhimu wa kutembelea vivutio vilivyopo katika hifadhi mbalimbali nchini na manufaa yake ikiwemo yale ya kiuchumi kwa taifa.

Alisema kuwa ziara hiyo ya wanahabari iwe chachu ya kuimarisha ushirikiano baina wahifadhi na wanahabari kwa lengo la kuibua mkakati wa pamoja katika kutangaza vivutio vilivyopo katika hifadhi za nchini Tanzania hususani vinavyopatikana katika hifadhi ya Taifa ya Ruaha ambayo ni hifadhi ya pili kwa ukubwa katika ukanda wa afrika.

Katika mazungumzo yake na Wataalii hao ambao ni wanahabari wa mkoani humo Kamishina msaidizi wa hifadhi ya taifa (RUNAPA), Godwell Ole Meng’ataki alibainisha kuwa wageni wanaotembelea hifadhi ya Ruaha upata fursa ya kujionea baadhi ya vivutio vya Kipekee ikiwemo Simba wanaishi kifamilia, wanyama wengine wa aina mbalimbali, utalii wa Ndege zaidi ya aina 574,  na Zaidi ya aina 1650 za mimea inayopatikana katika hifadhi hiyo pekee

Kamishina Meng’ataki alisema katika hifadhi ya Ruaha kuna aina mbalimbali za utalii ukiwemo utalii wa kutembea kwa miguu, utalii wa usiku, utalii wa boti na utalii wa uvuvi wa samaki huku akisisitiza kuwa aina hizo za utalii wa kipekee zikitangazwa kikamilifu zitachochea ongezeko la watalii katika hifadhi hiyo.

Alisema kuwa hifadhi ya Taifa Ruaha ni hifadhi yenye ualisia wake tofauti na hifadhi nyingine jambo ambalo linavutia watalii wengi kuitembelea.

Kiongozi huyo wa RUNAPA alizungumzia matokeo ya Filamu ya Royal Tour iliyoongozwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan ambayo aliitaja kuwa na mchango mkubwa katika kuutangazia Ulimwengu juu ya vivutio vilivyopo nchini huku akimpongeza Rais kwa kujitoa kwake katika kuchochea ukuaji wa sekta ya utalii wenye Tija.

Meng’ataki alisema kitendo kilichofanywa na Rais kinapaswa kuungwa mkono na kila mtanzania kama walivyofanya wanahabari wa mkoani Iringa walioungana na kufanya safari ya Utalii waliyoipa jina la Iringa Journalists Ruaha The Royal Tour ikiwa ni hatua ya wazi ya kutambua mchango wa sekta ya utalii nchini

Kwa upande afisa Uhifadhi katika hifadhi hiyo, Amina Rashidi alisema kuwa hifadhi ya Taifa ya Ruaha (RUNAPA) kwa mwezi Julai mwaka 2022 ilipata watalii 2,232,ikiwa ni ongezeko la watalii 532 kutoka 1,700 walioitembelea kwa mwaka mzima wa 2021.


Amina alisema kuwa ongezeko hilo la watalii limetokana na Royal Tour iliyosaidia kutangaza utalii nchini

“Royal Tour imesaidia kutangaza hifadhi zetu, baada ya korona watalii wameanza kurudi kwa sababu watalii wa nje hawakuwepo, tulikuwa tunapata watalii wa ndani lakini sasa tunapata watalii wengi wa ndani na nje,” alisema Amina.



Alisema hifadhi imeanza kupokea watalii kwa wingi, viwanja vya ndege vyote vinafanya kazi na mageti yana pilikapilika za wageni wa ndani na nje.

Naye mwenyekiti wa waandishi wa habari mkoa wa Iringa Frank Leonard alisema kuwa Waandishi wa habari Iringa wanatambua mchango wa utalii katika maendeleo ya taifa

Leonard alisema kuwa lengo la waandishi wa habari Iringa kutembelea hifadhi ya taifa ya Ruaha ni kuhakikisha wanahamasisha sekta ya utalii hasa watalii wa ndani ili wahamasikie kutembelea vivutio vya utalii vilivyopo hapa nchi.

Alisema kuwa waandishi wa habari wanaushawishi mkubwa wa kuhakikisha wanawashawishi wananchi wengine kwenda kutalii katika hafadhi ya Taifa ya Ruaha na hifadhi nyingine kupitia vyombo vya habari ambavyo wanavifanyia kazi.

Leonard alimazia kwa kusema kuwa mkakati uliopo kwa waandishi wa habari wa mkoa wa Iringa ni Kahakikisha wanatembelea vivutio vyote vya utalii vya nyanda za juuu kusini ili kupata elimu na kuvijua vivutio hivyo kwa lengo la kuanza kuvitangaza vivutio na hifadhi zote za taifa.

Share this:

Post a Comment

unashauriwa kutoa maoni muda na wakati wowote na kama unahabari yeyote unaruhusiwa kututumia

 
Back To Top
Copyright © 2014 MOUNT KILI NEWS. Designed by OddThemes | Distributed By Gooyaabi Templates