Ticker

6/recent/ticker-posts

AFUGWA MIAKA SABA KWA KUJERUHI KWA SILAHA

MAHAKAMA ya Hakimu Mkazi wilayani Babati mkoani Manyara imemhukumu mkulima mkazi wa kijiji cha Shambala wilayani Simanjiro mkoani Manyara Bw Ayubu Sanale kutumikia kifungo cha miaka saba gerezani baada ya kupatikana na hatia ya kujeruhi kwa silaha baridi.
Hukumu hiyo imetolewa janaNovemba 9 na Hakimu wa mahakama hiyo bw Kelanga Maginga baada ya kuridhika na ushahidi wa mashahidi wanne wa upande wa mashtaka uliotolewa kulingana na mwenendo mzima wa kesi hiyo huku mshtakiwa huyo akishindwa kuwasilisha mashahidi na kuamua kujitetea mwenyewe.
Akisoma jalada la mashtaka mwendesha mashtaka wa polisi Wahabi Mussa alisema mshtakiwa Ayub Sanale alitenda kosa hilo Januari 13 mwaka huu majira ya saa 1:00 Usiku katika eneo la kitongoji cha Endamtu Mirerani kwa kumvamia Rafiki yake Saidi Hassani  na kukata vidole vya mikono na miguu kwa lengo la kutaka kumpora fedha.
Ameendelea kuieleza mahakama hiyo kuwa siku hiyo kabla ya kujeruhiwa mlalamikaji alikutana na mshtakiwa huyo ambaye ni rafiki yake katika kitongoji hicho wakati alipokuwa akitokea eneo la KIA na kumwomba kumsindikiza kuelekea eneo la Mirerani lakini mshtakiwa alikataa na badala yake alimzunguuka.
“ mshtakiwa alimzunguuka rafiki yake na alishirikiana na rafiki yake kumsubiria mbele kabla ya kumvamia na kumkata vidole vya mkono wa kulia na vidole vya mguu wa kulia na kumsababishia ulemavu..alitenda kosa hili akiwa na mwenzake ambaye amekimbia nab ado anatafutwa na polisi”
 Aidha kabla ya kutolewa kwa hukumu hiyo upande wa mashtaka uliiomba mahakama hiyo kutoa adhabu kali ili iwe fundisho kwa watuhumiwa wengine kama hao hasa kutokana na kushamiri kwa vitendo vya uhalifu na unyang’anyi wa kutumia silaha huku upande wa utetezi ukiiomba mahakama hiyo kumhurumia kwa kuwa  ni yatima, na ana familia.
“mheshimiwa hakimu kwanza naomba mahakama itambue kuwa nimesingiziwa na mahakama naiomba inisamehe na adhabu inayotaka kunihukumu ama isitoe adhabu kali kwani mimi ni yatima,nina mke na motto wte hawa wananitegemea”
Hata hivyo baada ya utetezi Hakimu Kelanga Maginga alisoma hukumu kwa kumhukumu mshtakiwa huyo kutumikia kifungo cha miaka saba gerezani pamoja na adhabu ya kumlipa kiasi cha shilingi milioni moja.

Post a Comment

0 Comments