BREAKING NEWS

Monday, November 7, 2011

CHADEMA WAAMUA KULALA KATIKA VIWANJA VYA NMC HADI KIELEWEKE



Matukio ambayo wafuasi wa chama cha demokrasia na maendeleo CHADEMA walikuwa wanafanya nje ya mahakama wakati wakimsubiri mbunge wao Godbless Lema ambapo licha ya kukaa kwa masaa  zaidi ya nane lakini mbunge huyo akuletwa mahakamani hapo


 kila mmoja alikuja kwa kasi akiwa anataka ampokee mmbunge wake



Mhe. Freeman Aikaeli Mbowe, Mwenyekiti wa chama Taifa katika kati,Mhe. Dr. Wilbroad Peter Slaa , Katibu Mkuu wa chama wa kwanza kuliapamoja na mmbunge aliyeandamana nao ambaye ni mwanasheria Tundu Lissu wakibadilishana mawazo kabla ya kupanda jukwaani
 hatimaye Mwenyekiti alipanda kumwaga sera zake
 baadaye katibu akapanda na wakaamu kuwa kwakuwa polisi  na mahakama wamekataa kumuachia huru mmbunge wa jimbo la Arusha mjini Godbless Lema basi watakesha katika viwanja vya NMC hadi kieleweke
 wote hawa wanasema kuwa wanapigania uhuru na walikuwepo kwenye maandamano

msafara wa maandamano ulianza hivi na ulikuwa unaongozwa na Dr Slaa katibu wa Chadema
 +
 wafuasi wa CHADEMA wakiimba wanamtaka mmbunge wao ambaye leo hakufanikiwa kufikishwa mahakamani


Mhe. Freeman Aikaeli Mbowe, Mwenyekiti wa chama Taifa akiwaasa wananchi waelekee katika viwanja vya |NMC ambapo walikuwa wanafanya mkutano wa chama hicho hapo hivi leo




NDEREMO na vifijo walivyokuwa navyo wanachama wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) jana vilitumbukia nyongo baada ya mbunge wa jimbo la Arusha kushindwa kutoka katika gereza la Kisongo.
Umati wa wafuasi wa chama hicho ulianza pilikapilika za kwenda kwenye gereza hilo kwa lengo la kumpokea Lema ambaye yuko rumande kwa wiki moja sasa baada ya kuwepo kwa taarifa kuwa angepatiwa dhamana.
Hata hivyo shamrashamra hizo ziliingia dosari baada ya makundi hayo kukaa muda mrefu nje ya gereza hilo bila ya kuwepo kwa dalili za kuachiwa kwa mbunge huyo.
Wafuasi hao walianza maandalizi ya kumpokea mbunge majira ya saa mbili asubuhi wakiwa ndani ya vyombo vya usafiri walizunguka huko na kule kuhamasishana ili waende kumpokea mbunge huyo na baadaye wahudhurie kwenye mkutano uliofanyika katika viwanja vya NMC.
Ilipotimu majira ya saa sita mchana pasipo dalili zozote za kutoka kwa Lema msafara huo uliamua kuondoka eneo la gereza hilo huku ukigawanyika katika makundi mawili ambapo moja lilikwenda Mahakama Kuu ya Arusha na jingine likaelekea katika viwanja vya NMC.
Wakiwa katika eneo la mahakama, wananchi hao walizuiwa kuingia ndani na askari wa jeshi la polisi na kuishia lango kuu wakiwa hawajui hatma ya Lema.
Uwepo wa wafuasi hao katika mahakama hiyo kuliwafanya mahakimu kushindwa kutoka kwa hofu ya usalama wao licha ya kuwapo kwa askari polisi.
Majira ya saa nane mchana msafara wa Mwenyekiti wa CHADEMA Taifa, Freeman Mbowe, uliwasili mahakamani hapo na kuzusha shangwe kubwa miongo mwa wafuasi wa chama hicho.
Hata hivyo shangwe hizo hazikuweza kudumu kwani taarifa zilipatikana kuwa Lema hatoweza kuachiwa hadi Novemba 14.
Polisi walilazimika kumuomba Mbowe awasihi wafuasi wa CHADEMA wasifanye vurugu wala kuingia shemu ambako kesi zilikuwa zikiendeshwa jambo ambalo kiongozi huyo alilifanya.
Mbowe aliingia kwenye ofisi ya Msajili wa Mahakama na kukaa kwa muda ambapo alipotoka aliwapatia waandishi nakala ya barua iliyotolewa mahakamani hapo jana yenye kumbukumbu namba RM/VOL. 11/50 kwenda kwa wakili wa mbunge wa Arusha, Godbless Lema, Method Kimomogoro.
Barua hiyo iliyosainiwa na Hakimu Mkazi, Judith Kamara, anayesikiliza shauri hilo akiwataka wadhamini wa mshtakiwa wafike mahakamani hapo siku ya kutajwa kwa kesi hiyo Novemba 14, mwaka huu, saa 2.30 asubuhi ili kukamilisha taratibu za dhamana.
Kwa mujibu wa masharti ya dhamana yaliyowekwa na mahakama hiyo ambapo wadhamini wawili Sarah Mohamed na Halfan Rasuli walijitokeza mahakamani hapo kwa ajili ya kumdhamini.
Katika kile kinachodaiwa kuepusha vurugu katika mahakama hiyo, Mbowe alilazimika kuagiza aletewe gari lenye vipaza sauti ili aweze kuzungumza na mamia ya wananchi waliokuwa wameshinda mahakamani hapo wakimsubiri Lema.
Mbowe aliwaomba wananchi hao waongozane kuelekea viwanja vya NMC ili akawaeleze kwa kina kile kilichotokea.
Wakati Mbowe akiendelea kuongea liliingia gari lililokuwa na viongozi wengine akiwemo Katibu Mkuu wa CHADEMA, Dk. Willibrod Slaa na mwanasheria wa chama hicho, Tundu Lissu, hali iliyoamsha shangwe miongoni mwa wananchi hao.
Baada ya hapo, waliondoka kwa maandamano wakipita barabara mbalimbali za jiji hilo kuanzia mahakamani wakipita barabara ya Samora kisha ile ya Sokoine mpka viwanja vya NMC ambapo walifika majira ya saa 10 jioni na kupokewa na umati mkubwa wa watu.
Viwanja vya NMC
Wafuasi na viongozi wa CHADEMA walipofika kwenye viwanja vya NMC mvua kubwa ilikuwa ikinyesha lakini haikuwazuia kufanya mkutano huo.
Akizungumza katika mkutano huo, Lissu alisema juzi wakili wa Lema aliiandikia barua mahakama akiieleza kuwa mteja wake amekamilisha masharti ya dhamana na shauri lake lipelekwe mahakamani jana.
Lissu alisema kwa mujibu wa sheria, mahakama ilitakiwa kutoa hati maalumu itakayomuwezesha Lema kutoka magereza ili aende mahakamani ambapo angeachiwa kwa dhamana kwa kuwa tangu awali mahakama iliweka bayana kuwa dhamana iko wazi.
Slaa anguruma
Alisema Lema ni mbunge wa wananchi waliomchagua kwa kura zao ila anakatizwa katika utekelezaji wa shughuli za kibunge kila mara ikiwemo kuzuiliwa kufanya mikutano pamoja na kutembea na wananchi wake.
Slaa alibainisha kuwa Lema aliona hakuna sababu ya kuwa nje ilhali uhuru wake unaminywa na watawala ambao wamekuwa wakimfanyia fitna kila kukicha.
“Polisi, mahakama na serikali wanatakiwa waelewe wananchi wa Arusha wamekataa kunyanyasika na uvumilivu umefika mwisho, hivyo sasa wanafanya maamuzi magumu wakiamini hakuna mwenye haki miliki ya nchi hii. Tunamtaka Rais Jakaya Kikwete aelewe kuwa Tanzania ya watu wote, watafia hapo,” alisema.
Mbowe
Alisema watafanya mkesha katika viwanja hivyo, hawalali kwa ajili ya Lema bali hiyo ni ishara ya kukemea uonevu, ukandamizaji unaofanywa kwa wananchi na watawala.
Alisema wameanza siasa mpya za kutoogopa risasi, mabomu, mvua wala magereza, hivyo wananchi wawaunge mkono jambo hilo hasa kwa kukesha katika viwanja hivyo ili kufikisha ujumbe.
Aliwataka watu wazima wawarudishe watoto majumbani, na pale uwanjani hawafanyi vurugu yoyote hata wakipigwa na polisi.
“Wapigieni simu wake zenu wawaletee chakula na mashuka na wawaite marafiki zao kuungana nao katika kutetea haki,” alisema.
Polisi wanena
Kaimu Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Arusha, Akili Mpwapwa, alisema jeshi hilo halitawatawanya wala kuwaingilia wafuasi hao kwani mbavu ni zao na kila mmoja ana uamuzi wake.
“Tumewaona wanafunga mahema na taa, sisi hatutamgusa yeyote anayetaka kubebwa na abebwe, kila mmoja ana utashi wa kufanya mambo yake lakini wachunge wasivunje sheria za nchi,” alisema

Share this:

Post a Comment

unashauriwa kutoa maoni muda na wakati wowote na kama unahabari yeyote unaruhusiwa kututumia

 
Back To Top
Copyright © 2014 MOUNT KILI NEWS. Designed by OddThemes | Distributed By Gooyaabi Templates