Ticker

6/recent/ticker-posts

MADEREVA PIKIPIKI NA MAGARI WAPATIWA MAFUNZO


Madereva wa magari na pikipiki wa Tarafa ya Sunya Wilayani Kiteto Mkoani Manyara, wamepatiwa mafunzo ya kuendesha vyombo hivyo vya moto kwa lengo la kutokomeza ajali za uzembe zinazotokea kila wakati hapa nchini.

Akizungumza baada ya kumalizika kwa mafunzo hayo juzi, Ofisa wa polisi jamii Tarafa ya Sunya, Inspekta Said Alute alisema madereva waliohitimu ni kutoka  Kata za Sunya na Dongo na walifundishwa na wataalam kutoka taasisi ya Apex.

Inspekta Alute alitoa wito kwa washiriki wote waliohitimu mafunzo hayo ya udereva kutekeleza kwa vitendo yale yote waliyofundishwa na walimu, hivyo wakakate leseni baada ya kulipia fedha zao mamlaka ya mapato nchini (TRA).

“Kupitia Ofisa Tarafa ya Sunya, watendaji wa kata za Dongo na Sunya, wenyeviti, watendaji wa vijiji na wananchi kwa ujumla, wakuchukulie mafunzo haya kama mwanga wa kupunguza ajali zisizo za lazima zinazotokea,” alisema.

Alisema wahitimu hao wanatakiwa kuheshimu na kufuata sheria za usalama barabarani hapa nchini kwani kupitia mafunzo hayo watakuwa wamejengewa uwezo wa kutosha wa kuwa makini pindi wawapo barabarani.

Kwa upande wao baadhi ya washiriki wa mafunzo hayo walilishukuru jeshi la polisi na taasisi ya Apex kwa kuandaa mafunzo hayo, kwani hivi sasa wataweza kupatiwa leseni za udereva na kuondokana na usumbufu waliokuwa nao.

Mmoja kati ya washiriki wa mafunzo hayo Hamis Juma alisema ajali zinazotokea kutokana na uzembe au zinazoepukika, hivi sasa zitapungua kwenye Tarafa hiyo ya Sunya, kwani elimu hiyo itawanufaisha ipasavyo endapo ikitumika vizuri.

Post a Comment

0 Comments