Ticker

6/recent/ticker-posts

MFUGAJI APEWA SIKU 10 KUAMISHA MIFUGO YAKE

Mfugaji Gwarudaa Lele mwenye ng’ombe 1,800 amepewa siku 10 na wana kijiji wa Oltukai, Kata ya Esilalei, Wilayani Monduli Mkoani Arusha, kuondoka na mifugo yake kijijini hapo akidaiwa kuishi bila kuwa na kibali.

Wakizungumza na waandishi wa habari juzi, wana kijiji hao walidai kuwa Lele alipewa hifadhi ya muda kwenye kijiji hicho ila akanogewa na kutaka kuendelea kuishi katika kijiji chao ili hali hajapata ridhaa ya wananchi hao.

Mkazi wa kijiji hicho, Lazaro Mabengo akizungumza huku akiwa na jazba  alisema Lele alifika eneo hilo na kuomba sehemu ya kujihifadhi akiwa na ng’ombe 200 lakini ameng’ang’ania hadi kufikisha ng’ombe 1,800.

“Huyu mtu amekuwa chanzo cha migogoro na kero kubwa kwenye kijiji chetu, pia mifugo yetu imekosa malisho kutokana na yeye kuwa na mifugo mingi inayoleta matatizo kwa wafugaji wa kijiji hiki,” alisema Mabengo.

Kwa upande wake diwani wa kata ya Esilalei, Malunga Nangari alisema Lele alivamia eneo la mkazi wa kijiji hicho Lelukunya Kirina, lenye ukubwa wa ekari tatu lililopo karibu na eneo la umma lililotengwa kwa ajili ya malisho.

Nangari alisema mfugaji huyo anatakiwa kuondoka eneo hilo kwani hana kibali chochote kinachomruhusu kuishi hapo, kutokana na kuwa awali aliomba kuishi kwa muda mfupi kipindi cha ukame ila akanogewa na kukaa hadi sasa.

Hata hivyo, Lele akizungumza na waandishi wa habari alisema wivu, chuki na ubaguzi wa baadhi ya wakazi wa eneo hilo, ndiyo umesababisha afukuzwe kwenye kijiji hicho japo aliishi vizuri na kufuata taratibu zote za eneo hilo.

“Huu ni ubaguzi jamani sasa kama siyo mauaji ni nini, kwa sababu mimi ni mang’ati ndiyo wananifanyia hivi karibu kijiji kizima nilishawapa ng’ombe zangu lakini nashangaa leo wananifukuza mimi siondoki, niende wapi?” alihoji Lele.


Post a Comment

0 Comments