Ticker

6/recent/ticker-posts

WAKULIMA WAWEZESHWA

Vikundi vya wakulima 920 wa zao la ufuta wa Tarafa ya Mbugwe Wilaya ya Babati Mkoa wa Manyara, wamefaidika kiuchumi baada ya kuwezeshwa na shirika la Farm Africa, kwa kufanya kuwa zao tegemezi kwenye biashara.

Akizungumza juzi kwenye warsha ya wadau wa ufuta iliyofanyika wilayani Babati, Mratibu wa mradi wa ufuta wa Farm Africa, William Mwakyami alisema kati ya wakulima hao 920 wanaume ni 490 na wanawake ni 430. 

Mwakyami alisema wakati awamu ya pili ya mradi wa ufuta ikitarajia kufikia mwishoni mwezi Octoba mwaka huu, kupitia Farm Africa wameweza kuongeza kipato cha kaya kwa asilimia 20 na kuwaunganisha wakulima na masoko.

Hata hivyo, alisema japokuwa ufuta kutoka Tanzania una soko kubwa duniani kuliko nchi nyingine za bara la Afrika, lakini haulimwi kwa wingi kwani nchi ya Sudan ndiyo inayoongoza kwa kuzalisha kwa wingi zao la ufuta.

“Ufuta wetu ndiyo unaoongoza kwa ubora kuliko ufuta kutoka nchi nyingine hivyo tunatakiwa tujitahidi kulima zaidi kwani wenzetu Sudan japokuwa sehemu kubwa ni jangwa lakini wanalima ufuta mwingi,” alisema Mwakyami.

Naye, Ofisa kilimo wa Farm Africa, Tumaini Elibariki alisema miongoni mwa mafanikio ya wakulima hao ni kuongezaka kwa uzalishaji wa mbegu bora ya ufuta kutoka kilo 2,000 (tani 2) hadi kilo 11,180 (tani 11.18).

“Kilimo hiki kimesababisha kuongezeka kwa kipato kwa wakulima hao kutokana na uzalishaji wa ufuta kutoka sh728,669 hadi kufikia sh2 milioni na mawakala 10 wamewaelimisha wakulima wengi kutumia pembejeo za kilimo,” alisema Elibariki.

Post a Comment

0 Comments