Ticker

6/recent/ticker-posts

POLEPOLE AFURAHISHWA JINSI MATUMIZI YA MILIONI 500 ILIVYOTUMIKA MERU

Chama cha Mapinduzi (CCM) kimesema kimeridhishwa na matumizi ya Sh500milioni zilizotolewa na Serikali katika halmashauri 183 nchini kwa ajili ya ukarabati na ujenzi wa majengo mapya ya zahanati na vituo vya afya.
Kauli hiyo imetolewa leo Februari 25, 2018 na Katibu wa Itikadi na Uenezi wa chama hicho, Humphrey Polepole wakati ikikagua ukarabati unaoendelea katika kituo cha afya cha Usa-River halmashauri ya Meru wilayani Arumeru mkoani Arusha akiwa katika ziara yake ya kutembelea kaya masikini zilizowezeshwa na mfuko wa Tasaf
"Mnafanya kazi nzuri inaendana na kiwango cha ubora wa miradi na kile cha fedha zinazotolewa ambazo zinatokana na kodi za Watanzania,” amesema.
Mganga mkuu wa wilaya, Cosmas Kilasara amesema miradi ya wilaya hiyo inaendelea vyema na kuwanufaisha wananchi.
Miradi hiyo ilitambulishwa katika kikao cha menejimenti ya halmashauri (CMT), kikao cha kamati ya elimu, afya na maji na kikao cha kamati ya fedha, uongozi na mipango

Amesema Februari mwaka huu mradi huo ulitambulishwa kwenye baraza la madiwani na kazi kuanza kufanyika kwa ujenzi wa majengo mapya likiwemo jengo la upasuaji mkubwa.
Majengo mengine ni pamoja na maabara, wodi ya mama na mtoto, nyumba ya mtumishi inayojitegemea, jengo la kufulia, jengo la kuhifadhia maiti, tanki la kuhifadhia maji, tanuru la kuchomea taka pamoja na njia za kuunganishia majengo ambayo yote yapo katika hatua mbalimbali za utekelezaji wake
Aidha alitaja mradi huo kuwa unahusisha pia ukarabati wa majengo likiwemo jengo la wagonjwa wa nje, wodi ya wazazi, duka la dawa na jengo la utawala ambayo bado utekelezaji wake haujaanza.
Alisema hadi kufikia Februari 23 mwaka huu jumla ya Sh135.4 milioni zilikuwa zimeshatolewa kwa ajili ya ununuzi wa vifaa mbalimbali vya ujenzi na sehemu za gharama za ufundi.
Amesema pamoja na kiasi hicho cha fedha upo pia mchango wa nguvu kazi kutoka kwa wananchi wa kata ya Usa-River pamoja na vijana wa CCM kwa kuchimba misingi ya majengo ya maabara na jengo la nyumba ya mtumishi pamoja na kukusanya mawe unaofikia Sh1.2 milioni.

Post a Comment

0 Comments