Ticker

6/recent/ticker-posts

NAIBU WAZIRI WA MADINI MHE BITEKO AUTAKA UONGOZI WA CHUO CHA MADINI DODOMA KUJITATHIMINI

Naibu Waziri wa Wizara ya Madini Mhe Dotto Mashaka Biteko akisikiliza kwa makini maelezo kuhusu mashine zilizotolewa na wafadhili pasina kutumika kwa muda mrefu wakati alipotembelea Chuo cha Madini Dodoma leo 15 Januari 2018. Picha Zote Na Mathias Canal

Naibu Waziri wa Wizara ya Madini Mhe Dotto Mashaka Biteko akiwasili Chuo cha Madini Dodoma kwa ajili ya ziara ya kikazi, leo 15 Januari 2018.

Naibu Waziri wa Wizara ya Madini Mhe Dotto Mashaka Biteko akizuru katika Chumba cha uchenjuaji madini wakati alipotembelea Chuo cha Madini Dodoma leo 15 Januari 2018.

Naibu Waziri wa Wizara ya Madini Mhe Dotto Mashaka Biteko akikagua mashine mbalimbali wakati alipotembelea Chuo cha Madini Dodoma leo 15 Januari 2018.
Naibu Waziri wa Wizara ya Madini Mhe Dotto Mashaka Biteko akiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya viongozi wa Chuo cha Madini Dodoma leo 15 Januari 2018.

Na Mathias Canal, Dodoma

Uongozi wa Chuo cha Madini Dodoma kilichopewa ithibati kamili ya kutoa mafunzo ya umahiri yaani Competence Based Education and Training System (CBET) umetakiwa kujitathmini ikiwemo kutatua changamoto zinazokikabili chuo hicho ndani ya wiki mbili.

Kauli hiyo imetolewa na Naibu Waziri wa Wizara ya Madini Mhe Dotto Mashaka Biteko Leo 15 Januari 2018 alipotembelea chuoni hapo na kujionea hali ya ufanisi wa chuo hicho huku akikerwa na uduni wa utunzaji wa vifaa katika chumba cha maabara ya uchenjuaji wa madini.

Mhe Biteko alisema kuwa pamoja na changamoto lukuki walizoainisha katika taarifa ya chuo iliyosomwa na Kaimu Mkuu wa Chuo hicho Ndg Vincent Willium Pazzia ikiwa ni pamoja na uchache wa bajeti, uhaba wa wakufunzi katika fani za uhandisi na usimamizi wa mazingira migodini na upungufu wa ofisi za watumishi, wanatakiwa kuwa na mikakati ya kukabiliana nazo ndani ya wiki mbili zitakazofika ukomo mwishoni mwa mwezi huu.

Alisema kuwa serikali ya awamu ya tano inayoongozwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe Dkt John Pombe Magufuli haitatoa fedha mahali ambapo hakuna matokeo ili ziliwe na watu wasiokuwa na matakwa mema na Taifa.

Aliongeza kuwa katika Wizara ya madini kumekuwa na malalmiko mengi kuliko utendaji jambo ambalo lisipotafutiwa ufumbuzi wa kudumu haraka litabakisha usugu na uvivu wa kufikiri kwa baadhi ya watendaji na kusalia kufanya kazi kwa mazoea pasina kuwa na ubunifu.

Naibu Waziri wa Madini Mhe Biteko alisema kuwa wakati Taifa likiwa linaelekea kuwa katika uchumi wa kati na mapinduzi ya viwanda huku rasilimali za madini zikipewa umuhimu mkubwa ni lazima watendaji wakubali kukabiliana na changamoto mbalimbali kwani tiba ya changamoto hizo ni pamoja na kuzikabili na kuzipatia ufumbuzi wa haraka.

Aidha, ameutaka uongozi wa chuo hicho cha madini kuhakikisha kuwa kinazalisha wataalamu wengi katika sekta ya madini ambao watalisaidia Taifa kutekeleza majukumu muhimu ya serikali ikiwemo uzalendo na ulinzi wa mali za umma.

Alisema kuwa watendaji wote serikalini wanapaswa kutambua kuwa wana jukumu kubwa moja la kuhakikisha kuwa wanatekeleza kwa ubora na umakini mkubwa maelekezo rasmi ya serikali ambayo yamebainishwa katika ilani ya uchaguzi ya Chama Cha Mapinduzi katika kipindi cha mwaka 2015-2020.


Post a Comment

0 Comments