Ticker

6/recent/ticker-posts

SERIKALI YADHAMIRIA KUIMARISHA HUDUMA KWA WAGENI WANAOINGIA NCHINI KUPITIA UWANJA WA NDEGE WA KIMATAIFA WA DAR ES SALAAM (JNIA)





Na Hamza Temba-Dar es Salaam

...................................................................................

SERIKALI kupitia wizara zake nne tofauti imedhamiria kukabiliana na changamoto mbalimbali za utoaji wa huduma kwa wageni wanaiongia na kutoka nchini kupitia Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Mwalimu Julius K. Nyerere (JNIA) jijijini Dar es Salaam.

Changamoto hizo ni pamoja na msongamano na joto katika eneo la kuchukulia mizigo, muda mrefu wa upatikanaji wa hati za kusafiria kwa wageni wanaoingia nchini pamoja na changamoto ya ufinyu wa eneo la kusubiri huduma uwanjani hapo.

Mawaziri wa Wizara hizo ambao wamefanya ziara ya pamoja katika uwanja huo jana na kukagua shughuli za utoaji huduma ni Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk. Hamisi Kigwangalla, Waziri wa Mambo ya Ndani, Dk.Mwigulu Nchemba, Naibu Waziri wa Mambo ya Nje Dk.Susan Kolimba na Naibu Waziri wa Ujenzi na Mawasiliano, Mhandisi Atashasta Nditiye.

Akizungumza uwanjani hapo, Dk. Kigwangalla alisema wamefikia hatua ya kukutana mawaziri hao baada ya wageni hasa watalii wanaiongia nchini kulalamika kuwa wanatumia muda mwingi kuhudumiwa katika eneo la uwanja huo kiasi cha kuwapotezea muda.

Dk.Kigwangala amesema kutokana na malalamiko hayo ya muda mrefu na mengine kadhaa hatua mbalimbali zimechukuliwa tangu Agosti 8 mwaka 2017 manaibu waziri wa wizara hizo nne walipofanya ziara uwanjani hapo kwa ajili ya kutafuta ufumbuzi changamoto hizo na kwamba kukutana kwao jana ni muelendezo wa kushughulikia kero hizo ambapo mafanikio yameanza kuonekana.

Dk.Kigwangala amesema ipo haja ya kuweka mikakati ya kuboresha huduma katika viwanja vya ndege nchini ukiwamo JNIA huku akisisitiza umuhimu wa watendaji na watoa huduma katika nafasi mbalimbali kuwa wakarimu kwa wageni.

Amesema ni vema hata Polisi walioko uwanjani hapo wakimkamata mgeni basi badala ya kutumia nguvu wawe na ukarimu kwani ni muhimu kumdhibiti mgeni bila kutumia nguvu ili ikibainika hana kosa aachiwe na asiwe na malalamiko ya kunyanyaswa.

Dk.Kigwangala amesema kuna haja kwa wageni wanapokuja Tanzania wakirudi makwao wasimulie ukarimu na uzuri wa nchini yetu. 

Ameongeza anatamani kuona kuanzia uwanjani hapo hadi hotelini ambako mgeni anakwenda anatumia muda mchache, anapata nafasi ya kuona picha za viongozi mbalimbali ambazo zitakuwa uwanjani, picha za wanyama na video ambazo zinaonesha utalii wa Tanzania.

Amesema kumpokea mgeni jambo moja lakini namna ya kumhudumia ni jambo jingine na ndilo muhimu zaidi na akafafanua hata teksi ambayo mgeni ataitumia kusafiri dereva awe na ukarimu hata wa kumsalimia na wakati mwingine kutabasamu.

Kwa upande wake, Waziri wa Mambo ya ndani Ndani Dk. Mwigulu Nchemba akizungumza baada ya ziara hiyo alisema jitihada mbalimbali zinafanywa kutatua changamoto hizo.

Ametaja hatua ambazo wizara yake inachukua ni kuharakisha utoaji huduma wa hati za kusafiria kwa njia ya kieletroniki.

Pia wameamua kuongeza idadi ya madawati ya kutolea huduma kwa wageni ikiwa sambamba na kuongeza watoaji huduma ili kurahisisha utoaji huduma wa muda mfupi.

“Taarifa zinaonesha kuwa kwa sasa kuna unafuu mkubwa wa kutoa huduma kwani badala ya saa tatu ambazo zilikuwa zinatumia awali hivi sasa muda wa utoaji huduma umeshuka hadi saa moja, lengo letu ni kushuka zaidi.

“Mbali ya kuboresha huduma tutahakikisha pia tunaongeza ulinzi na usalama katika viwanja vyetu vyote nchini ili kudhibiti wageni wenye nia ovu na nchi yetu.

“Tunafahamu mataifa mengi yameitikia mwito wa uwekezaji nchini hasa katika mikakati ya kufikia Serikali ya Viwanda na uchumi wa kati.
“Hivyo wageni wanakuja kwa nia njema ya kuwekeza lakini hatutaki wale wenye nia mbaya kutumia mwanya huo.Hivyo tutaendelea kuimarisha ulinzi na usalama katika viwanja vyetu,”amesema.

Kwa upande wa Naibu Waziri wa Mambo ya Nje, Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Kikanda na Kimataifa, Dk. Susan Kolimba amesema wanaridhishwa na hatua ambazo zinachukuliwa katika kuondoa changamoto zinazoelezwa kuwapo uwanjani hapo.



Amesema wizara yao inatamani kuona idadi ya wageni inaongezeka zaidi na wakati huo huo wakifurahia huduma ambazo wanazipata wakifika nchini kwetu. Alisema Wizara yake itaendelea kuitangaza Tanzania na vitutio vyake ili idadi ya watalii iweze kuongezeka.

“Tumefanya ziara na binafsi niseme tu nimeridhishwa na hatua ambazo zinachukuliwa katika kuondoa changamoto hizo,”amesema Dk.Kolimba.

Naye, Naibu Waziri wa Ujenzi na Mawasiliano, Mhandisi Atashasta Nditiye amesema wizara yao tayari imechukua hatua mbalimbali za kuondoa changamoto zilizopo ikiwamo ya kufunga viyoyozi (AC) kwa ajili ya kuondoa hali ya joto.

“AC zilizopo ni za muda mrefu kwani ziliwekwa tangu majengo ya uwanja huo yalipojengwa. Hivyo tayari zimeanza kufungwa AC mpya na ndio maana joto limepungua” amesema.

 Pia amesema wamepata kampuni ambayo itakayofanya ukarabati kwa kuongeza eneo la kukaa wageni wanaosubiri huduma mbalimbali kabla ya kutoka uwanjani.

Amesema kuna jitihada mbalimbali Serikali inafanya jitihada za kuondoa msongamano wa wageni ikiwamo ya kuharakisha ujenzi wa jengo jipya la kusafiria wageni la Terminal III ambalo litahudumia watu milioni sita badala ya jengo la sasa ambalo wakati linajengwa  lengo lake lilikuwa kuhudumia watu milioni moja.

“Ujenzi wa jengo jipya umekamilika kwa asilimia 70 na litakapokuwa tayari kwa asilimia 100 litaanza kutumika kwa kuwa kasi ya ujenzi inakwenda vizuri,’amesema.


 Waziri wa Maliasili na Utalii Dkt. Hamisi Kigwangalla akiteta jambo na Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi Dk. Mwigulu Nchemba wakati wa ziara ya pamoja ya kukagua Changamoto mbalimbali wanazokumbana nazo wageni hususan watalii  wanaoingia nchini kupitia uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Dar es Salaam JNIA jana kwa ajili ya kukabiliana nazo.

Waziri wa Maliasili na Utalii Dkt. Hamisi Kigwangalla akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es salaam jana wakati wa ziara ya pamoja ya kukagua Changamoto mbalimbali wanazokumbana nazo wageni hususan watalii  wanaoingia nchini kupitia uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Dar es Salaam JNIA kwa ajili ya kukabiliana nazo. Wengine walioshiriki ziara hiyo ni Waziri wa Mambo ya Ndani, Dk. Mwigulu Nchemba (wa pili kulia), Naibu Waziri wa Ujenzi na Mawasiliano, Mhandisi Atashasta Nditiye (wa tatu kulia) na Naibu Waziri wa Mambo ya Nje, Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Kikanda na Kimataifa, Dk. Susan Kolimba (wa nne kulia).
 Waziri wa Maliasili na Utalii Dkt. Hamisi Kigwangalla (wa pili kulia) akiteta jambo na  Naibu Waziri wa Mambo ya Nje, Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Kikanda na Kimataifa, Dk. Susan Kolimba jijini Dar es salaam jana wakati wa ziara ya pamoja ya kukagua Changamoto mbalimbali wanazokumbana nazo wageni hususan watalii  wanaoingia nchini kupitia uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Dar es Salaam JNIA kwa ajili ya kukabiliana nazo. Wengine walioshiriki ziara hiyo ni Waziri wa Mambo ya Ndani, Dk. Mwigulu Nchemba (wa tatu kushoto) na Naibu Waziri wa Ujenzi na Mawasiliano, Mhandisi Atashasta Nditiye (wa pili kushoto) .
 Waziri wa Maliasili na Utalii Dkt. Hamisi Kigwangalla (wa tatu kulia) akiteta jambo na  Naibu Waziri wa Mambo ya Nje, Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Kikanda na Kimataifa, Dk. Susan Kolimba jijini Dar es salaam jana wakati wa ziara ya pamoja ya kukagua Changamoto mbalimbali wanazokumbana nazo wageni hususan watalii  wanaoingia nchini kupitia uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Dar es Salaam JNIA kwa ajili ya kukabiliana nazo. Wengine walioshiriki ziara hiyo ni Waziri wa Mambo ya Ndani, Dk. Mwigulu Nchemba (kulia) na Naibu Waziri wa Ujenzi na Mawasiliano, Mhandisi Atashasta Nditiye (wa pili kulia).


Post a Comment

0 Comments