Ticker

6/recent/ticker-posts

SIKUTOA LESENI YA VITALU VIPYA: MAGHEMBE


Image result for VITALU VYA WANYAMA

WIZARA ya Maliasili na Utalii imetoa ufafanuzi kuwa, Waziri wa Wizara hiyo, Profesa Jumanne Maghembe hakutoa leseni za umiliki wa vitalu vipya, bali ameongeza muda wa umiliki wa vitalu kwa mujibu wa sheria na kanuni.
Ufafanuzi huo unatokana na habari iliyoandikwa na gazeti la Raia Mwema la Januari 25-31 Januari 2017, lililodai kuwa waziri Maghembe anadaiwa kuongeza muda wa leseni za vitalu vya uwindaji kwa kampuni za uwindaji wa kitalii kinyume na taratibu.
Taarifa kwa vyombo vya habari iliyotolewa na Katibu Mkuu wa Wizara hiyo jana, ilieleza kuwa waziri alifanya hayo chini ya Kifungu cha 38 (8) cha Sheria ya Kuhifadhi Wanyamapori Namba 5 ya mwaka 2009 sambamba na Kanuni ya 16 ya Kanuni za Uwindaji wa Kitalii za mwaka 2015.
“Sheria na Kanuni hiyo inaelezea utaratibu wa kuongeza muda wa umiliki wa vitalu kwa wale walioomba kuendelea na umiliki wa vitalu vya awali,” ilieleza sehemu ya taarifa hiyo.
Taarifa hiyo alifafanua kuwa Waziri kabla ya kuongeza muda wa umiliki wa vitalu, alikaribisha maombi kwa wanaotaka kuongezewa muda huo na maombi hayo yalipitiwa na Kamati ya Ushauri ya Ugawaji wa Vitalu vya Uwindaji iliyopo kisheria na iliteuliwa Septemba 2013 na kumshauri waziri.
Alisema uongezaji wa muda wa umiliki wa vitalu vya uwindaji ulifuata sheria, kanuni na taratibu.
“Hivyo tunawaomba wananchi wapuuze habari hiyo, kwani mwandishi alikusudia kuupotosha umma kwa kunukuu na kutafsiri vifungu vya Sheria ya Kuhifadhi Wanyamapori isivyo sahihi”.
“Habari hiyo siyo ya kweli, kwani Waziri hakutoa leseni za umiliki wa vitalu vipya bali ameongeza muda wa umiliki wa vitalu kwa mujibu wa Kifungu cha 38 (8) cha Sheria ya Kuhifadhi Wanyamapori Namba 5 ya mwaka 2009 na Kanuni ya 16 ya Kanuni za Uwindaji wa Kitalii za mwaka 2015,” ilieleza taarifa hiyo.

Post a Comment

0 Comments