Ticker

6/recent/ticker-posts

SHILINGI MILIONI 20 ZADAIWA NA WAFANYABIASHARA WA SUNGURA KWA KAMPUNI YA THE RABBIT BLISS


 


WAFANYABIASHARA wa sungura zaidi ya 20 mkoani Arusha, wameilalamikia Kampuni ya Mradi wa Sungura ya The Rabbit Bliss Limited ya jijini Arusha kwa kushindwa kuwalipa madai yao ya zaidi ya Sh milioni 20 baada ya kuuziwa sungura wa nyama na wafugaji hao.
Wafugaji hao wameeleza kupanda mbegu za sungura hao katika Mradi wa Ufugaji wa Sungura katika kampuni hiyo yenye ofisi zake Ngaramtoni, nje kidogo ya Jiji la Arusha, kama ambavyo wamekubaliana kwenye mkataba kwa lengo la kujipatia fedha baada ya mauzo ya sungura, lakini hali imekuwa fofauti.
Wakizungumza kwa nyakati tofauti katika ofisi hizo jana, wafanyabiashara hao walijiunga mwaka jana katika kampuni hiyo kwa lengo la kuiuzia kampuni hiyo kwa makubaliano ya Sh 8,000 kila kilo moja ya nyama ya sungura na kwamba malipo hufanyika kila baada ya wiki mbili.
Mmoja wa wafugaji hao, Godson Makundi alisema alijiunga ndani ya mradi huo mwaka jana na kununua majike watano wa sungura pamoja na dume moja kwa gharama ya Sh 950,000 katika kampuni hiyo na kwenda kuwafuga.
Makundi alieleza kwamba baada ya muda, alizalisha jumla ya sungura 21 aliowawasilisha mbele ya kampuni hiyo kwa lengo ya kupatiwa kiasi cha fedha, lakini cha ajabu hajalipwa fedha zake mpaka sasa.
“Nilileta jumla ya sungura 21 zenye kilo 55 na niliambiwa baada ya wiki mbili nitalipwa fedha zangu, lakini cha ajabu hadi sasa sijalipwa chochote,” alisema Makundi.
Lawrence Mosha alisema alijiunga ndani ya mradi huo mwaka jana na alinunua na kuuza jumla ya sungura 50 kwa kampuni hiyo kwa kiasi cha Sh milioni moja, lakini hadi sasa anasotea malipo yake.
Mfugaji mwingine, Joseph Minja alisema alilipia mbegu 57 za sungura kwa gharama ya Sh milioni tano na kuahidiwa kupatiwa sungura hao, lakini hadi sasa hajapata chochote.
Akijibu malalamiko hayo kwa njia ya simu, Mkurugenzi wa kampuni hiyo, Payas Ruben alisema kumekuwa na mabadiliko ya uongozi wa kampuni yao, ambayo kwa kiasi kikubwa yamechangia kuibua migogoro baina yao na wateja mbalimbali.
Alisema wakati akikabidhiwa kampuni hiyo, Novemba mwaka jana kutoka kwa mkurugenzi wa awali ambaye ni raia wa Kenya aliyemtaja kwa jina moja la Mtuwa, alikuta akaunti ya kampuni hiyo ina Sh milioni mbili pekee, hivyo kwa sasa wameanza kujipanga upya na watafanya malipo ya wafanyakazi hao ndani ya miezi mitatu kuanzia sasa.
Alisema baadhi ya wafugaji hao hawana mikataba na kampuni kutokana na baadhi yao kufanya makubaliano na malipo nje na taratibu.

Post a Comment

0 Comments