Kutokana na walimu wa shule ya sekondari Mwandeti iliyopo katika halmashauri ya Arusha mkoani Arusha,kuzalisha rasilimali watu nakuleta matokeo chanya kwa jamii,Wazazi kwa kushirikiana na jamii wamenunua gari aina ya costa ili kupunguza adha ya walimu hao kutembea umbali mrefu kufika katika kituo chao cha kazi.
Wakizungumza baada ya kununua usafiri huo shuleni hapo,Baadhi ya wazazi Lotegerwaki Merusori na Loivy Ngailova walisema kutokana na changamoto ya ukosefu wa nyumba za walimu katika eneo la shule wameamua kununua gari kama sehemu ya shukrani kwa kile wanachozalishiwa kwa watoto wao.
Walisema walimu wanawafundishia watoto wao vizuri na wanafauli hivyo hawana budi kuwashukuru kwa kuwapunguzia baadhi ya changamoto kama ya usafiri kwani nyumba za walimu katika eneo la shule hazitoshelezi.
"Shule yetu hii ya sekondari Mwandeti inakabiliwa na changamoto ya nyumba za walimu na kutokana huduma ya elimu wanayotoa na kutoa matokeo chanya kwa watoto wetu tumeamua kununua gari hili litakalokuwa linawabeba walimu wote kwa wakati mmoja na kufika kituo cha kazi kwa muda muhafaka kufundisha wanafunzi,"alisema Mzazi Ngailova.
Naye Mkuu wa shule ya sekondari ya Mwandeti John Massawe alisema wazazi na jamii waliyafurahia matokeo ya wanafunzi wa kidato cha nne na sita hali iliyowapelekea kununua gari kama sehemu ya kuwashukuru walimu kwani wanakabiliwa na nyumba za walimu ambapo ziliopo ni tisa kati ya walimu 51.
Aliongeza kuwa baada ya wazazi kuona changamoto hiyo wakatafakari hata wakijenga nyumba moja itamnufaisha mwalimu mmoja hivyo wakaona wanunue usafiri utakaowanufaisha walimu na wanafunzi kwa pamoja.
"Kweli tuna uhaba wa nyumba za walimu shuleni hapa ikiwa wengi wao huishi mbali na shule kutokana na wazazi wao wenyewe kuweka ahadi juu yetu kwamba tukiondoa ziro shuleni kwetu watatufanyia kitu kikubwa hivyo tunawashukuru wazazi hao kwa kutimiza ahadi yao kwetu na sisi tunawahaidi tutafanya kazi kweli kweli,"alisema Mwalimu Massawe.
Vilevile alisema wanawashukuru wazazi hao kwa kujitolea kununua usafiri huo kwani ni dhahiri wameonyesha namna wanavyowajali walimu wa watoto wao hivyo ushirikiano utakuwa endelevu katika kuleta maendeleo ya shule pamoja na ya wanafunzi.
Mwalimu Massawe alisema pia anaishukuru serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Rais wa jamuhuri ya muungano wa Tanzania Samia Suluhu Hassan kwa uboreshaji wa miundombinu ya shule na ufaulu utaongezeka kutokana na wanafunzi hawatabanana tena kwenye mabweni na kupunguza msongamano katika madarasa.
Pia aliiomba serikali iwasaidie kutatua changamoto ya maji kwa ni wanafunzi na walimu wanapata tabu ya upatikanaji wa maji kwani kwa sasa wanatumia mfumo wa kuvuna maji ya mvua.
Kwa upande wake Mkurugenzi wa Halmashauri ya Arusha,Suleiman Msumi amewataka wazazi katika shule nyingine kuiga mafano huo kuisaidia serikali katika kutekeleza majukumu yake.
0 Comments
unashauriwa kutoa maoni muda na wakati wowote na kama unahabari yeyote unaruhusiwa kututumia