RC AUNDA KAMATI YA KUCHUNGUZA WALIOGOMA KUJIUNGA NA MAMLAKA YA MJI MDOGO WA NGARAMTONI




Wananchi wa Kitongoji cha Saitabau, Kata ya Tarakwa wilaya ya Arumeru,Mkoa wa Arusha, wamegoma kujiunga na Mamlaka ya mji mdogo wa Ngaramtoni na kuruhusu mradi wa maji katika kijiji chao kuwa chini ya Mamlaka hiyo.

Kutokana na mgomo huo, Mkuu wa mkoa wa Arusha, Mrisho Gambo ameamua kuunda kamati ya wataalam kutoka ofisini kwake ili kuchunguza mgogoro huo.
Wakizungumza na Mkuu wa mkoa wa Arusha, Mrisho Gambo  aliyefika katika kitongoji hicho, kukagua mradi wa maji wa Olosaita  uliokwama, ikiwa ni sehemu ya ziara yake ya siku tano katika halmashauri ya Arusha vijijini, wananchi hao walisema hawataki kujiunga na Mamlaka hiyo kwani hawajuwi faida zake.

Mwenyekiti wa kitongoji hicho,Lucas Lukumai alisema wananchi wanapinga kujiunga na Mamlaka hiyo, kutokana na kutopatiwa elimu na pia mamlaka kutaka kuchukuwa mradi wao wa maji ambao waliuchangia na kusaidia na shirika la Oxfam.

"Mimi nilikamatwa na kuwekwa rumande na polisi kwa agizo la Mkurugenzi  wa halmashauri kwa tuhuma za kukataa mamlaka jambo ambalo sio kweli wanaokataa ni wananchi wenyewe kwani hawajapewa elimu"alisema
Alisema viongozi wa Mamlaka walipewa fursa ya kukutana na wananchi na kutoa elimu lakini wameshindwa kufanya hivyo, badala yake wanawatuhumu viongozi.

Akijibu tuhuma hizo, Mtendaji mkuu wa Mamlaka ya mji mdogo, Sophia Shoko alisema wananchi wanagomea kujiunga na mamlaka kwa lengo la kuzuia mradi wa maji usiwe chini ya Mamlaka yao.

"hapa kuna mradi wa maji, wenyewe hawataki uwe chini ya Mamlaka ili maji yasambazwe maeneo mengine na wanataka kuendelea na malipo ya sh 500 kwa mwezi jambo ambalo sio sahihi"alisema.

Hata hivyo, Diwani wa kata hiyo, Elihuruma Laizer alimuomba Mkuu wa mkoa kuunda kamati maalum ya kuchunguza suala hilo na atafute fursa ya kukaa na wananchi kuwasikiliza kwani jambo hilo lina mgogoro mkubwa.

Akizungumza baada ya majadiliano hayo, Mkuu wa mkoa wa Arusha, Mrisho Gambo alisema anakubaliana na ushauri wa Diwani wa kata  hiyo, kuunda kamati maalum ya kuchunguza mgogoro huo kabla ya kuchukuwa hatua.

"nitaunda kamati ya wataalam kutoka ofisini kwangu watakuja hapa na kuzungumza na wananchi , viongozi wa Mamlaka ya mji mdogo na viongozi wa kitongoji  na baadaye watanipa ushauri kufikia maamuzi"alisema.

Mamlaka ya mji mdogo wa Ngaramtoni, iliundwa mwaka jana na halmashauri ya Arusha vijijini ili kupeleka huduma za kiserikali karibu zaidi na wananchi .

Post a Comment

unashauriwa kutoa maoni muda na wakati wowote na kama unahabari yeyote unaruhusiwa kututumia

Previous Post Next Post